The House of Favourite Newspapers

Wolper, Sarakasi za Mapenzi Zinakuharibia

0
Muigizaji Jackline Wolper na baby wake, mwanamitindo anayeitwa Brown

MIONGONI mwa mambo ambayo napenda kuyafanya nje ya kazi yangu ya uandishi, ni kutazama filamu. Kwenye eneo hili ninao uzalendo wa kuringia kwani nimejikita sana kuangalia sinema za hapa Bongo, ingawa zipo nyakati huwa najikuta nikinogewa na uigizaji wa wasanii wa nje, kutegemeana na aina ya filamu na maudhui yake.

 

Kwa mantiki hiyo, wapo wasanii wachache hapa Bongo ambao nawakubali kwa uwezo wao wanapokuwa wakikamua kazi mbele ya kamera, miongoni mwao ni pamoja na mdogo wangu, Jacqueline Wolper.

Jackline Wolper na Harmonize.

Aliingia kwenye game la Bongo Movie, tayari kabati langu la stoo likiwa limejaa filamu nyingi za Kitanzania nilizokwisha kutazama,  naye akafanya yake na kunishawishi kumkubali.

 

Kwa jinsi alivyo kikazi, Jack anajua kucheza na akili za watazamaji wenye macho ya uchambuzi na upembuzi wa mambo kama mimi. Pia msanii huyu ni kati ya wanawake wachache sana waigizaji wetu wenyekupambana na maisha kwa kiwango kikubwa, anayo kiu kubwa sana ya mafanikio na ndiyo maana amekuwa akiruka huku na kule kusaka noti kwa kutoka jasho halali.

Pamoja na hayo, lipo jambo moja ambalo mdogo wangu asipolitazama kwa jicho la ziada, linaweza kumuondolea kabisa sifa yake ya upambanaji wa maisha kama msanii na mjasiriamali. Ni upande wa pili wa maisha yake, yaani mapenzi. Eneo hili Jack amekuwa na sarakasi nyingi sana ambazo zimenifanya leo nifikirie kumpa ushauri kupitia hapa kwani muda wangu wa kukutana naye kama nilivyosema hapo juu, ni mdogo na ni wa kubahatisha mno.

Wolper na Mkongo.

Mlolongo wa maisha yake ya mahusiano umejaa dosari za namna ambayo hailingani kabisa na hadhi na nafasi aliyonayo katika jamii pamoja na umri kwa jumla. Nimewahi kufanya mahojiano fulani na Jack ambapo alinibainishia umri wake halisi, ni kweli bado ni binti mdogo sana, tofauti kabisa na namna ambavyo watu wengi wanamfikiria, lakini lazima ajue kuwa kila siku usomaji wa kalenda unabadilika.

Amekuwa mtu wa kuingia kwenye mahusiano ya kimapenzi, tena mara nyingi na vijana wadogo kabisa anaowaacha mbali kiumri na kuishia kuumizwa kwa kuachwa hivyo kuongeza orodha na idadi isiyokuwa na maana katika historia ya maisha yajayo.

Niseme tu kuwa, Jack una sifa nyingi nzuri mno, lakini tatizo ni nini linalokufanya ushindwe kuwa na utulivu kwenye anga la mapenzi? Kama ni urembo unao? Jina maarufu unalo na kwa upande wa pesa sina shaka juu ya hilo kutokana na mambo ninayoyaona ukiyafanya kwa juhudi za mikono yako, tatizo lako ni nini mdogo wangu? Hebu kaa chini ujiulize mara mbilimbili. Muda haukusubiri kwa chochote.

Hayo mambo ya sijui umeiba mume wa mtu, mara umepora mpenzi na mchumba wa mwanamke fulani, yanaharibu mno mustakabali wa maisha yako yajayo, kwani historia inayo

tabia ya kudumu milele hata kama mhusika ataondoka chini ya jua. Au una shida gani kwenye eneo hilo la mapenzi? Uliwahi kufanya mahojiano na mmoja wa waandishi wetu, ukamwambia wanaume wote uliowahi kuwa nao kwenye mahusiano hawana matatizo, ila wewe ndiye ‘mshenzi’ na kwamba huabudu mapenzi hivyo ukimchoka mtu unamuonesha njia na hujawahi kuachwa! Sasa mambo gani hayo?

Yaani kweli uzuri wote wa sura ulionao nao, ujuzi wa kazi na upambanaji wa kimaisha ulionao, kumbe ndani si chochote? Sitaki kuamini kama na wewe una ule uzuri wa mkakasi kumbe ndani ni kipande cha mti. Ni wakati wako sasa kubadilika na kuwa Wolper mpya, kutulia na mwanaume unayeendana naye, kufunga naye ndoa na kisha kutengeneza familia na kuyaacha maisha yasonge kwa heshima zake.

 

Leave A Reply