ILIPOISHIA
“Sawa. Lifunge ulichukue.”
Mganga akalifunga sanduku hilo lililokuwa wazi kisha akalibeba na kuliweka begani.
SASA ENDELEA
“
Mimi naenda zangu,” mganga huyo akaniaga mara tu alipoliweka sanduku hilo begani. Macho yake yalikuwa yakimeta kwa tamaa ya pesa.
“Utaweza kwenda nalo hadi kule kijijini kwenu?” Nikamuuliza.
“Hili litafika bila wasiwasi wowote.”
Hapo hapo nikakumbuka kitu. Niliukumbuka ule mkoba nilioukuta mvunguni mwa kitanda cha marehemu ambao ndani yake mlikuwa na vitu vya ajabu.
“Hili sanduku lilikuwa pamoja na mkoba fulani, ngoja nikakuletee,” nikamwambia na kuongeza.
“Mimi hautanihusu tena.”
“Uko wapi?” Mganga akaniuliza.
“Ngoja nikakuchukulie, uko chumba kingine.’
Nilidhani mganga angelitua lile sanduku ili asubiri nikamchukulie huo mkoba lakini alibaki na sanduku lake begani, akaniambia.
“Kaulete. Nakungoja.”
Nikatoka katika kile chumba. Mganga naye alitoka. Nilipoingia katika chumba cha marehemu, mganga huyo alisimama pale pale ukumbini na sanduku lake.
Niliutoa ule mkoba chini ya kitanda cha marehemu baba yangu nikaukung’uta vumbi kisha nikatoka nao.
“Huu hapa,” nikamwambia yule mganga huku nikimpa mkoba huo.
Nilidhani mganga huyo angetaka kuufungua ili aone vilivyokuwa ndani lakini hakuufungua, akaniambia.
“Haya naenda zangu.”
“Sasa kwa upande wangu hakutakuwa na matatizo tena?” nikamuuliza.
“Matatizo nitakuwa nayo mimi. Wewe hutakuwa na matatizo tena.”
“Na wale watu wangu kule kwenye pango itakuwaje?”
“Wale waache kulekule. Kesho asubuhi tutakwenda sote ili niwashughulikie. Watakuwa wazima.”
“Kwa hiyo kesho asubuhi nikusubiri hapa nyumbani?”
“Ndiyo nisubiri nitakuja na vifaa vyangu. Wewe endelea tu kuwapelekea chakula.”
Mganga aliponiambia hivyo alikuwa akivuka kizingiti cha mlango wa mbele.
Nilimuona ana haraka. Nikamwambia.
“Basi tutakutana hapo asubuhi.”
“Sawa.”
Mganga akaanza kuchapuka akiwa na sanduku hilo begani. Nilisimama barazani nikimtazama alivyokuwa akitembea kwa kasi. Akilini mwangu nilimsifu. Mganga huyo kiafya alikuwa dhaifu dhaifu lakini alikuwa amepata nguvu za ghafla kiasi kwamba aliweza kulibeba lile sanduku na kwenda nalo kwa kasi.
Sikuzijutia zile pesa. Mawazo yangu yalikuwa kwa mama yangu na mwanangu. Kama alivyoniambia yule mganga, pesa ni tamu lakini masharti yake yalikuwa magumu. Kwa vyovyote vile nisingeyaweza na kama ningeingia tamaa ya kutaka kumiliki pesa hizo, zingenisumbua.
Ningeweza kupata kichaa au kufa kabisa.
Baada ya yule mganga kupotea kwenye macho yangu nilirudi ndani nikaingia chumbani mwangu. Niliketi kitandani huku kichwa changu kikiwaza hiki na kile.
Nilivyokuwa ninataka mimi, mama yangu na mwanangu walioko kule kwenye pango watolewe haraka na kushughulikiwa.
Maneno ya yule mganga kwamba tusubiri hadi kesho asubuhi twende naye pamoja, hayakunifurahisha lakini sikuweza kumpinga kwa sababu yeye ndiye mtaalam.
Nilihisi mama yangu na mwanangu wanapoendelea kukaa katika lile pango, walikuwa wakiendelea kuteseka na kunikosesha furaha. Kusema kweli sikuwa na furaha hata chembe kila nilipowakumbuka. Nilikuwa nikipata majonzi yasiyomithilika.
Tena niseme ukweli kifo cha baba yangu kamwe hakikunihuzunisha hasa vile nilivyogundua kuwa alimfanyia ukatili mama na mwanangu.
Nikatamani nirudi tena kule pangoni nikawaone. Nikatoka uani nikatayarisha uji mwingine na kuutia asali kisha nikautia kwenye chupa.
Ile chupa niliitia kwenye mfuko nikatia na vikombe viwili kisha nikaanza safari ya kuelekea kule pangoni.
Nilipoingia kwenye lile pango niliwaona wale watu wamelala fofofo. Walikuwa wanakoroma na kutoa mlio wa kutisha. Nilijaribu kuwaamsha lakini hawakuamka. Nikaamua kukaa nao hadi watakapoamka wenyewe.
Yalipita karibu masaa matatu nikiwa kwenye pango hilo. Nilikuwa nimeketi kimya nikiwatazama watu hao kwa huruma huku nikimuwaza baba yangu kuwa alikuwa mtu katili sana.
Sikuwa na shaka yoyote kuwa muda ule alikuwa akionja adhabu ya Mwenyezi Mungu huko ahera alikokuwa.
Baada ya masaa matatu ndipo watu hao walipoamka. Nilihisi kama walikuwa na kiu ya maji kwani walikuwa wamezitoa nje ndimi zao zilizokuwa zinatoka ute.
Laiti ningekuwa na maji ningewapa lakini sikuwa na maji ya kunywa. Nikaona niwatilie ule uji wanywe. Nilipowatilia uji huo walikunywa kwa pupa ingawa ulikuwa moto. Kila mmoja alikunywa vikombe vitatu.
Nilipohisi kuwa walikuwa wameshiba, moyo wangu uliridhika kidogo.
Nikaondoka hapo pangoni na kurudi nyumbani nikiwa mnyonge sana. Nilipofika nilifikia kulala tu. Niliamka saa mbili usiku nikaenda kuoga kisha nikarudi tena kulala. Siku ile sikula chakula cha jioni.
Ilikuwa kama majira ya saa sita hivi nilipoamshwa usingizini wakati mlango wa mbele ulipobishwa kwa kishindo.
Nikatoka ukumbini kisha nikauliza.
“Nani abishaye?”
“Mimi mganga. Tafadhali nifungulie.” Sauti ya yule mganga ikasikika huko nje.
Itaendelea wiki ijayo
HADITHI ZA KUSISIMUA NA MBINU ZA UJASIRIAMALI, INGIA NA LIKE PAGE YA FACEBOOK YA ERIC SHIGONGO===>https://www.facebook.com/shigongotz/
KWA HABARI ZA KITAIFA, KIMATAIFA, MASTAA NA MIKASA YA KUSISIMUA TUFOLLOW
INSTAGRAM===>https://www.instagram.com/globalpublishers/
TWITTER===>https://twitter.com/GlobalHabari
FACEBOOK===>https://www.facebook.com/GlobalPublishers
SUBSCRIBE YOU TUBE===>https://www.youtube.com/user/uwazi1