Gladness Mallya, Amani
DAR ES SALAAM: Bila huruma! Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeliingiza sokoni lile gari la kifahari aina ya Range Rover Evouge la Miss Tanzania 2006, Wema Sepetu kwa madai ya ukwepaji wa kodi, Amani limetonywa!
Kwa mujibu wa chanzo chetu kutoka ndani ya TRA, Ofisi Kuu jijini Dar es Salaam (long room), Evouge la Wema liko mnadani kinachosubiriwa ni tarehe ya kuita wateja kwa ajili ya manunuzi.
KISA CHA MNADA
“Lile gari linaonesha liliingia nchini kutoka Msumbiji ambako mtu wa kwanza alikuwa ni Mussa Anli akiwa na makao nchini humo.
“Lakini baada ya kufika kwa Wema likaonekana kutokuwa na uhalali wa kuwepo nchini, hasa kwa upande wa mapato ya nchi. Likakamatwa na mmiliki wake (Wema) alipewa siku za kulipa, hajafanikisha hilo. Kwa hiyo likawa liko nchini kinyume na utaratibu (overstayed), ndiyo maana TRA imeamua kuliuza ili fedha za mapato ziingie serikalini.”
SIKU YA MNADA
Chanzo: “Mnada utafanyika Julai 18, mwaka huu kule bandarini kwenye warehouse (ghala la kuhifadhia bidhaa). Kwa hiyo kila kitu kitakuwa pale. Itakuwa Jumapili kuanzisa saa 4 asubuhi na kuendelea.”
MASHARTI YA UNUNUZI
Chanzo: “Mtu atakeyeshida mnada, atatakiwa kulipa asilimia 25 on the spot (papohapo) halafu asimilia 75 itakayosalia lazima ilipwe ndani ya saa 48 tangu kufanyika kwa mnada.
“Lakini pia, gari litatakiwa kuondolewa eneo la mnada baada ya mnunuzi kumaliza kulipa asilimia 75 iliyobaki.”
GAZETI LA SERIKALI
Chanzo chetu kilikwenda mbele kwa kusema kuwa, TRA imefuata taratibu zote za uuzaji wa gari hilo kwani kupitia Gazeti la Serikali la Daily News la Juni 16, mwaka huu, ilitangaza mnada huo kama sheria inavyotaka.
WATEJA WATEMBELEA
Kwa mujibu wa chanzo hicho, baadhi ya wateja wameanza kutembelea eneo hilo ili kujionea gari hilo ambalo ni jipya katika matumizi.
MBALI NA GARI LA WEMA
Hata hivyo, chanzo chetu kilisema kuwa, mbali na gari la nyota huyo, bidhaa nyingine mbalimbali zitapigwa mnada kwa watu watakaopenda kununua, kama TV, magari, mafuta ya kupikia na mifuko ya sukari.
WEMA AMEFIKAJE HAPA?
Katika sherehe yake ya siku ya kuzaliwa ‘bethidei’, Novemba mwaka jana, (kawaida ni Septemba 28), Wema alitangaza hadharani kwamba, alilinunua gari hilo kwa dola za Kimarekani 90,000 (zilikuwa si chini ya shilingi milioni 200) huku akisema ni mali yake.
ILIANDIKWA
Hata hivyo, siku chache baadaye, gazeti hilihili liliandika kwa kufuata chanzo kimoja kutoka TRA kikinyetisha kwamba, kasi ya Rais John Pombe Magufuli ‘JPM’ kuhakikisha hakuna Mtanzania anayekwepa kulipa kodi, gari hilo la kifahari linachunguzwa na mamlaka hiyo.
WASIWASI WA VIPATO
Chanzo hicho kilisema kuwa, uchunguzi wa gari hilo pamoja na mengine ya mastaa wa Bongo, ulitokana na mamlaka kuwa na wasiwasi na usahihi wa kulipa kodi kwa sababu ya maisha yao ya kifahari huku vipato vyao vikiwa haviko wazi.
ALIKAMATWA
Januari mwaka huu, Wema akiwa na gari hilo maeneo ya Aficana, Mbezi-Beach jijini Dar wakati akiwa anakwenda kwenye bethidei ya rafiki yake aliyefahamika kwa jina la Kibadude, alikamatwa na watu wa TRA kwa makosa ya kuliendesha bila vibali na kubainika kuwa, lilikuwa na ‘figisufigisu’ katika uhalali wa kuingia nchini.
KIGOGO ALIMUOKOA
Hata hivyo, katika sakata hilo, kiogozi mmoja serikalini aliwaambia watu wa TRA kumpa siku saba msanii huyo kuwasilisha nyaraka bila kuliendesha gari hilo kinyume cha siku hizo, lichukuliwe na TRA kwa ajili ya mnada jambo ambalo lilitimia na sasa gari hilo lipo manadani.
MKURUGENZI WALIPA KODI
Baada ya madai hayo, Amani lilimtafuta Mkurugenzi wa Elimu kwa Walipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo ili kumsikia anasemaje kuhusu hilo lakini simu yake iliita bila kupokelewa.
WEMA ASAKWA JUZI
Ili kuweka sawa mzani wa habari, juzi Jumanne, Amani lilimpigia simu Wema lakini iliita bila kupokelewa. Alipopigiwa simu mtu mmoja wa karibu yake, alisema haikuwa rahisi kwa Wema kupokea simu kwani alikuwa Uwanja wa Taifa, Dar kuangalia mpambano wa Timu ya Yanga na TP- Mazembe kutoka DRC.

