Mtoto Miriam akionesha majeraha.
Na Issa Mnally, UWAZI
DAR ES SALAAM: Ofisi ya Ustawi wa Jamii Wilaya ya Kinondoni, imemhifadhi Miriam (10) baada ya kuona akinyanyaswa kupita kiasi na mama yake (jina linahifadhiwa), ambaye ni mkazi wa Kimara jijini Dar es Salaam.
Mjumbe wa Shina Na. 063 Mavurunza A, Mtaa wa Kwakichwa, Janet Moshi amethibitisha kuchukuliwa kwa mtoto huyo, baada ya wazazi wake kukimbia nyumba yao na kupotelea kusikojulikana baada ya kuanza kutafutwa na polisi.
Mtoto Miriam baada ya kupata hifadhi.
Mjumbe huyo alidai kuwa kutokana na unyanyasaji ambao amekuwa akifanyiwa, hata mahudhurio ya binti huyo shuleni yamekuwa hayaridhishi. Baada ya kumuokoa kutoka kwenye mikono ya wazazi hao, majirani pamoja na mjumbe huyo walimpeleka polisi.
Mmoja wa majirani wa binti huyo aliyejitambulisha kwa jina la Donata, aliliambia gazeti hili kuwa mtoto huyo hivi sasa yupo katika mikono salama ya serikali akilelewa na ustawi wa jamii na anaendelea vizuri.
“Yule mama na mumewe wametoroka, wanatafutwa ili washtakiwe, hatujui wamekimbilia wapi,” alisema mama huyo na kulimwagia sifa Gazeti la Uwazi kuwa ndilo lililofanikisha mtoto huyo kuchukuliwa na serikali.