
BONDIA: Mfaume Mfaume ambaye ndiye aliyepambana ulingoni na bondia Mohammed Rashid Matumla aliyelazwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili akiendelea na matibabu baada ya kupasuliwa fuvu la kichwa, ameelezea kuhusu pambano hilo na jinsi alivyomjeruhi Matumla.

Akizungumza katika mahojiano maalum na Global TV Online, Mfaume alisema kabla ya pambano hilo, alijiandaa vizuri kwa kufanya mazoezi makali na magumu na hata kabla pambano halijaanza, alijua lazima atamshinda Matumla.

Anaeleza kuwa baada ya pambano hilo kuanza, alianza kumpiga mpinzani wake ngumi kalikali, lakini naye akawa anamjibu, ikawa ni ‘piga nikupige’ mpaka raundi ya saba alipomuwasha ngumi kali, iliyomfanya apoteze mwelekeo.

“Nilipompiga nilijua hawezi kuinuka, lakini alijikaza na kuinuka tena ingawa bado alikuwa amelewa kwa ile ngumi, nikaendelea kumshambulia na baadaye, mwenyewe alisalimu amri,” alisema Mfaume na kuongeza:




“Hata hivyo hayakuwa malengo yangu kumuumiza kiasi kile, nilitegemea ataanguka na baada ya muda atakuwa sawa, nasikitika sana kwa yaliyotokea lakini ni sehemu ya mchezo maana hata yeye angeweza kunipiga ngumi kali nikaumia. Namuombea kwa Mungu apone haraka na tupo pamoja kwenye hiki kipindi kigumu,” alisema.