
KIKOSI cha Everton kupitia kocha wao, Ronald Koeman, kimesema kimefurahia ziara yao nchini Tanzania iliyobebwa na ukarimu wa watu wake tangu walipowasili hadi walipomaliza mechi yao na Gor Mahia.
Everton inayoshiriki Ligi Kuu England, ilikuwepo nchini kwa ziara maalum iliyoratibiwa na wadhamini wao Kampuni ya Michezo ya Kubahatisha ya SportPesa ambayo pia inaidhamini Gor Mahia ya Kenya.

Juzi Alhamisi, Everton ilicheza mechi ya kirafi ki na Gor Mahia ambao ni mabingwa wa michuano ya SportPesa Super Cup kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kushinda mabao 2-1.
Mabao ya Everton yalifungwa na Wayne Rooney dakika ya 35 na Kieran Dowell aliyefunga dakika ya 45 huku bao la Gor Mahia likifungwa dakika ya 37 na Jacques Tuyisenge.

Baada ya mchezo huo, Koeman alisema: “Ni ziara nzuri kwetu na tumeifurahia Tanzania, tumekaa muda mfupi lakini tumefurahia maisha hapa kwa mapokezi mazuri. Nimefurahi sana na kuwa Tanzania.” Akizungumzia mchezo dhidi ya Gor Mahia, Koeman alisema: “Ulikuwa mzuri, ulivutia na ushindani ulikuwa mzuri. Nimeipenda mechi hii ya kirafi ki na ulikuwa mchezo mzuri kwetu.”