
KATIKA kuhakikisha wachezaji wake wanakuwa na fiziki ya kutosha, kocha Mkuu wa Yanga Mzambia, George Lwandamina, jana aliwakimbiza wachezaji wake nyota kwa dakika 90 uwanjani.
Wakati Lwandamina akifanya hivyo alitumia muda mwingi kupambana na kiungo wake, Papy Tshishimbi ambaye mara kwa mara alikuwa akimuita na kumpa maelekezo tofauti na wachezaji wengine.

Hiyo yote ni katika kujiandaa na mechi ijayo ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Singida United, itakayochezwa Jumamosi hii kwenye Uwanja wa Namfua mkoani Singida.
Yanga itaingia uwanjani katika mechi hiyo kuvaana na Singida ikiwa imetoka kupata sare ya bao 1-1, dhidi ya Simba mchezo uliochezwa wikiendi iliyopita kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar.
Katika mazoezi hayo, mbali na Papy, Lwandamina alionekana kuwakomalia wachezaji wengine nyota akiwemo, Ibrahim Ajibu, Obrey Chirwa na Kelvin Yondani katika kuhakikisha wanakuwa fiti kwenye mechi hiyo.
Kocha huyo, alianza programu ya mazoezi saa 3:00 na kumalizika saa 4:30, zikiwa ni dakika tisini kwa kukimbia huku wakizunguka uwanja mzima.
Katika mazoezi hayo, kocha huyo aligawa makundi ya wachezaji waliokuwa wakikimbia na kupumzika sekunde kumi kabla ya kupuliza filimbi iliyokuwa ikiwaongoza nyota hao huku jua likiwa kali uwanjani hapo.
Kocha huyo, aliweka kituo kimoja wakati wakiendelea kukimbia ambako ilikuwepo mipira miwili na kila kundi likifika hapo, basi walitakiwa kuchezea mpira kwa kuunyanyua kwa sharti la kutoanguka chini.
Mara baada ya programu hiyo kumalizika kocha huyo aliwataka wachezaji hao kwenda kunywa na maji.
Katika mazoezi hayo, walikosekana wachezaji watatu pekee ambao ni majeruhi, Amissi Tambwe, Thabani Kamusoko na Donald Ngoma.