WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harryson Mwakyembe leo ametangaza majina wajumbe 25 wa Kamati ya Maandalizi kuelekea michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Vijana (Afcon 2019).
Akizungumza na wanahabari leo Jumamosi jijini Dar es Salaam, Mwakyembe amesema wajumbe wote walioteuliwa wamethibitisha uteuzi huo na hivyo hakuna hata mmoja wao aliyekataa uteuzi huo.
“Naomba mjue kuwa, mwaka 2019 siyo mbali kuelekea michuano hii ya Afcon kwa vijana, hivyo ili tuweze kujiandaa vizuri imenibidi nichague wajumbe wa kamati ya maandalizi mapema,” alisema
Miongoni mwa wajumbe walioteuliwa ni katika kamati hiyo ni Dk Damas Ndumbaro, Francis Michael, Mohamed Dewji, Abdallah Bakhresa, Yusuf Singo, Ahmed Mgoyi, Dk Hamis Kigwangala na Dk. Deotha Mdachi.

Amesema wajumbe wote 25 walioteuliwa watakuwa chini ya mwenyekiti wao, ambaye ni yeye mwenyewe Mwakyembe, makamu wake akiwa ni Leodegar Tenga na Mkurugenzi wa Kamati atakuwa Henry Tandau.