
UKIZUNGUMZIA soka la Tanzania ni ngumu kuzikwepa klabu kongwe za Simba na Yanga ambazo zinaongoza kwa kuwa na mashabiki wengi kuliko timu nyingine zinazoshiriki Ligi Kuu Bara.
Kwa upande wa viongozi wa soka, jina la Hassan Dalali nalo ni maarufu kutokana na kujijengea heshima kwenye mchezo huo alipokuwa kiongozi wa Simba.
Dalali ni mmoja kati ya wale wazee wa zamani wa Msimbazi, aliyeshika nyadhifa kadhaa kabla ya kuwa kiongozi wa juu wa Simba. Anafahamika kuwa ni mwenye mapenzi ya kweli na klabu hiyo.
Anajulikana kwa kutokuwa na makuu, lakini mwenye mipango na huenda alikuwa akidharaulika kwa kigezo kwamba hajaenda shule kwa kiwango cha kuitwa msomi kabla ya hivi karibuni kuamua kurejea darasani kupiga kitabu upya lakini amebarikiwa hekima na busara.
Mara zote kiongozi huyo amekuwa mtu wa watu, ukipata bahati ya kupiga naye stori za hapa na pale utagundua jambo hilo, ni mcheshi, anapenda utani kwani kuna majina amepachikwa na mwenyewe anayafurahia.
Championi Ijumaa linakuchambulia majina hayo katika makala haya ambayo amekuwa akiitwa kiongozi huyo na wadau mbalimbali wa Simba na mchezo wa soka hapa nchini huku mengine akijipa mwenyewe:
FIELD MARSHAL (FM)
Maana halisi ya jina hili ni cheo cha mwisho au cha juu kabisa katika jeshi. Mashabiki wa Simba walimpa jina hilo kutokana na kumuona ni kiongozi shupavu, anakumbukwa kwa kuiwezesha klabu hiyo kununua eneo linalotarajiwa kujengwa uwanja wa mazoezi lililopo Bunju nje kidogo ya Jiji la Dar.
Mashabiki wa Simba wameendelea kumuita jina hilo wakati wote na mwenyewe amekuwa akilifurahia kutokana na heshima aliyojijengea kwenye timu hiyo kuanzia 2006 hadi 2010 alipokuwa mwenyekiti kwenye klabu.
HANDSOME BOY (HB)
Kwa lugha rahisi maana yake ni mvulana mtanashati ambaye wakati wote anakuwa kwenye mwonekano nadhifu, hivyo ndivyo ilivyo kwa Dalali ambaye mara nyingi hupenda kutupia kanzu yake nyeupe, koti na kibalaghashia.
Licha ya umri wake kuwa mkubwa mwenyewe anapenda kuitwa kwa jina hilo la Handsome Boy au HB kama anavyoitwa na mashabiki wa timu hiyo kutokana na mwonekano wake ikizingatiwa hivi karibuni amemaliza elimu yake ya kidato cha nne.
TRUMP
Anakumbukwa na wengi kwa kuwa enzi zake akiwa mwenyekiti wa Simba alikuwa akiinyanyasa Yanga ambao ni wapinzani wakubwa wa Simba.
Dalali akiwa kiongozi wa Simba alikuwa akiifunga Yanga mara nyingi kasoro mwaka 2008 ambapo Benard Mwalala alifunga bao lililoipa ushindi timu hiyo ya Jangwani.
Mashabiki wa Simba wanamfananisha kiongozi wao huyo wa zamani na rais wa sasa wa Marekani ambaye ni rais wa 45 katika taifa hilo, Donald Trump, sababu kubwa wote ni watu wa misimamo mikali.
S a b a b u nyingine ya m a s h a b i k i wa timu hiyo kumpachika jina hilo ni kutokana na kiongozi huyo kuamini katika kusimamia jambo la kweli na lenye maendeleo kama ilivyo kwa Trump mwenyewe anayepinga matumizi ya nguvu za nyuklia.
KIM JONG-UN
Mashabiki wa Simba wanadai wakati wa utawala wa Dalali ndani ya timu hiyo alikuwa mtata hasa dhidi ya watani zao Yanga, wakaona siyo kesi wakaamua kumpachika jina la Rais Korea Kaskazini, Kim Jong-un.
Dalali mwenyewe anatajwa kuwa mmoja wa viongozi waliowahi kutokea kwenye timu hiyo wakiwa wenye msimamo mkali kama ilivyokuwa sasa kwa rais wa Korea Kaskazini ambaye ni mtoto katika uzao wa Kim Jog-il (rais wa pili wa Korea Kaskazini) na kwa sasa ndiye kiongozi wa nchi hiyo, alichukua cheo hicho baada ya kifo cha baba yake, Desemba 2011.
DALALI MWENYEWE HUYU HAPA:
Alipoulizwa Dalali kuhusu majina hayo alikiri kuyatambua na kusema hawezi kuyakataa kwa kuwa ni sehemu ya mchezo anaoupenda wa soka.
“Ni majina ambayo nakutana nayo kila siku, naitwa jina fulani kutegemea na eneo nililopo lakini kwangu hayana tatizo na ninayakubali tu,” anasema.