
JUZI Jumatatu moja ya mambo ambayo nilikuwa nikiyafikiria ilikuwa ni juu ya mwelekeo wa Yanga lakini hasa ni kuhusu aliyekuwa Kaimu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Clement Sanga.
Nilijuliza inakuwaje Sanga anaendelea kuwa kiongozi wa klabu hiyo wakati inaelekea shimoni na hakukuwa na dalili nzuri za kuinusuru inapoelekea klabu na timu kwa jumla.
Sanga ni mmoja wa viongozi wazoefu kwenye soka la Tanzania, anazo sifa za kuwa kiongozi mzuri japokuwa kuna wakati huwa nawaza yawezekana kukaa kwake chini ya kivuli cha Yusuf Manji ndiko kuliko mfanya aonekane kiongozi mzuri, Labda!
Tangu kuondoka kwa Manji, Yanga ilionekana kukosa mwelekeo mzuri, timu na klabu kwa jumla vyote vilianza kupoteza dira na ikaonekana kama nguvu ya kumtegemea mtu mmoja ndiyo iliyokuwa ikiwatafuna Yanga.
Juhudi za hapa na pale zikawa zinafanyika, lakini kuondoka kwa Manji kukafumbua mambo mengi na kuonyesha walijisahau na kuamini Manji ni Yanga na Yanga ni Manji, hivyo hawakuwa tayari kisaikolojia kujiandaa kuishi bila Manji ambaye alitangaza kujiuzulu nafasi yake.
Manji aliondoka Yanga mwaka jana, lakini juzi kwenye mkutano wa wanachama wakapinga kujiuzulu kwake wakimuomba arejee, hapo unaweza kujiuliza kwanza kwa kipindi chote ambacho Sanga alikaimu alionyesha wazi hana uwezo wa kuwa mwenyekiti na ndiyo maana wanachama wakaomba Manji arejeshwe.
Hilo lilikuwa ‘tusi’ kubwa kwa Sanga hata kama na yeye alitaka Manji arudi kama inavyosemwa, kwa kitendo hicho pekee kinaonyesha kuwa Sanga hakuwa akitosha kwenye viatu vya kuwa bosi mkubwa katika taasisi hiyo kubwa.
Achana na hayo, ndani ya muda mfupi ambao amekaimu uongozi, ameshindwa kuifanya klabu kuwa na umoja, makundi yamekuwa mengi na kila mtu amekuwa na nguvu ya kusema hiki na kile, kuamua hiki na kile.
Unapokuwa kiongozi wa juu kisha ukashindwa kudhibiti watu wako wa chini kufanya maamuzi kiholela na mbaya zaidi yakawa na hasara kwa taasisi, hiyo inamaanisha umeshindwa kuongoza.
Sanga wakati akitangaza kujiuzulu alielezea kufuatwa nyumbani na watu waliokuwa na mapanga na silaha nyingine za jadi, hilo hata mimi nalipinga halikuwa sawa na ninalikemea kwa nguvu zote.
Kuna wapuuzi wachache ambao bado wanaamini kubishana kwa kuumizana kwa silaha ndiyo njia ya kufikisha ujumbe wakati unaweza kutumia hoja, kwa hilo lililotokea pole sana Sanga.
Sanga huyuhuyu ameonyesha wazi kushindwa kuendesha timu, hata kama klabu siyo mtu mmoja bado hiyo haiondoi uhalisia kuwa yeye ndiye mwenye mamlaka ya juu ya uongozi na anayo mamlaka ya kuwaonyesha njia wengine wa chini yake ili wamfuate.
Klabu imekuwa ikilia njaa, mikataba ya wachezaji inaisha hakuna juhudi za kueleweka zilizokuwa zikifanyika, Sanga aliacha mambo yaende kama zile zama za zamani za kila mdau kusajili mchezaji wake, ndiyo maana ikaundwa ile kamati maalum ya kina Abbas Tarimba.
Tangu wiki iliyopita nilieleza kuwa sikuwa na imani na kamati hiyo na nilijua haitakuwa na mwisho mzuri kwa kuwa ilikuwa ikibeba majukumu ya watu ambao wapo kwenye uongozi na ndiyo majukumu yao, kwa asili ya soka letu nilijua ni vita, na ndicho kilichotokea.
Wakati yote hayo yakiendelea kutokea Sanga alitumia muda mwingi kuwa kimya, kama alikuwa akifanya matukio ya uongozi basi ilikuwa ni ya ndani ambayo hayana faida wakati mambo yameshakuwa mabaya hadharani.
Unapoona kuna mgogoro unafukuta au unakuwa mkubwa kwenye taasisi kisha kiongozi wa juu yupo kimya, huku kukiwa na malalamiko mengi juu yake mwisho wake huwa ni mbaya.
Mbali na hapo, katika picha ya kawaida tu Sanga alionyesha hakuwa na nia ya dhati ya kuiongoza Yanga ambayo kwa sisi watu wa soka tunajua jinsi ambavyo soka linavyoweza kuwa kama imani kwa watu, hivyo, namtakia Sanga safari njema.
Kwa ufupi nimwambie tu hakuwa na uwezo wa kuvaa viatu vya kuwa bosi namba moja wa klabu hiyo na kujiuzulu kwake siyo kwa bahati mbaya, ilikuwa lazima itokee.
Na Vuvuzela na John Joseph