






MAHAFALI ya kwanza ya Shule ya Jovin Junior Nursery yamefana kwa wanafunzi wa shule hiyo kuonekana wakiwa wamependeza na kusherehekea, tayari kwa ajili ya kujiunga na elimu ya msingi mwakani.
Mahafali hayo yalifanyika leo asubuhi katika shule hiyo iliyopo maeneo ya Salasala jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi katika sherehe alikuwa ni Afisa Elimu wa Kata ya Salasala, Fauster Tutu.
Akizungumzia katika mahafali hayo, afisa elimu huyo aliwaomba wazazi wazingatie suala la kuwapatia watoto elimu bora kwa kuwajengea msingi mzuri wa elimu bora kama inayotolewa na shule hiyo.
Kwa upande wao wazazi, waliishukuru shule hiyo kwani imewasaidia watoto kuwa na msingi mzuri ambao utawasaidia kuanza darasa la kwanza wakiwa wanajua kusoma na kuandika kwa ufasaha.
Meneja wa shule hiyo, Meshack James amewashukuru wazazi waliojitokeza katika mahafali hayo na amewataka wazidi kuunga mkono suala la elimu hasa kwa watoto wakati angali wadogo.
“Niwashukuru na nitoe wito kwa wazazi wengine, wawalete watoto wapate elimu kwani sisi tunawalea vizuri watoto katika maadili,” alisema Meshack.