POLISI mkoani Kagera imeanza uchunguzi wa kifo cha aliyekuwa katibu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Kata ya Katoke wilayani Muleba Jaspar Jasson (41) ambaye mwili wake ulikutwa kando kando ya barabara asubuhi ya, Februari 17, 2020, huku ukiwa na michubuko ya kamba shingoni.
Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Revocatus Malimi, amesema kuwa mwili huo umekutwa na dalili zote za kunyongwa au kujinyonga lakini kinacholeta utata ni eneo ulipokutwa, kwa kuwa hakuna mti wala alama zinazoonyesha kuwa tukio limetokea katika eneo hilo.
Kwa mujibu wa Malimi, Jasson alionekana hadharani kwa mara ya mwisho Februari 16, mwaka huu, saa kumi na moja jioni katika kijiji cha Bisore alikohamia baada ya kutelekeza familia yake na kwenda kuishi na mwanamke mwingine na kwamba upelelezi kuhusiana na tukio hilo umeanza, huku akiwaomba wananchi kutoa ushirikiano kwa polisi.
