WADHA-MINI wa Yanga ambao ni Kampuni ya GSM, wamerejea kwa kishindo na sasa wameweka wazi mipango yao ya kujenga uwanja mkubwa wa kisasa wa kuchezea mechi za Ligi Kuu Bara na mashindano mengine pamoja na hostel za wachezaji.
Kauli hiyo wameitoa ikiwa ni siku chache tangu kampuni hiyo kuandika barua kujiweka pembeni kwa kuacha kutoa bonasi kwa wachezaji, mishahara, kusafirisha timu na gharama za kambi baada ya kutofautiana na baadhi ya viongozi wa Kamati ya Utendaji ambao baadaye walijiuzulu katika nafasi zao.
Yanga kama wakifanikisha hilo la kujenga uwanja huo wa kuchezea basi watakuwa wamewazidi watani wao Simba waliojenga viwanja viwili vya kufanya mazoezi vilivyokuwepo Bunju, Dar ambavyo vilijengwa na mwekezaji wao Mohammed Dewji ‘Mo’.
Kwa kupitia Ofisa Muhamasishaji wa timu hiyo, Antonio Nugaz alisema kuwa kwa sasa wanachama na wapenzi wa Yanga wajiandae kupata furaha kwani mengi yanakuja baada ya GSM kurejea kwa kishindo mara baada ya kutangaza kujiweka pembeni.
Nugaz alisema kuwa tofauti na uwanja huo wa mechi, pia utajengwa mwingine utakaotumika kwa ajili ya mazoezi kwa timu zao za vijana na wanawake utakaokuwa na mabwawa ya kuogelea Kigamboni, Dar es Salaam.
Aliongeza kuwa kikubwa wanataka kuifanya Yanga iwe ya kimataifa zaidi ya hapo ilipofikia na hilo linawezekana kwao kutokana na uwepo wa wadhamini wao GSM wanaosimamia zoezi zima la usajili hivi sasa ambao tayari wamefanikisha kumbakisha Mghana Bernard Morrison.
“GSM itajenga uwanja wa kuchezea mechi kabisa na siyo wa mazoezi kama walivyofanya watani wetu, Simba na utakuwa na kila kitu kinachohitajika katika uwanja wetu huo utakaokuwa wa kisasa.
“Wanayanga wafahamu kuwa GSM imerejea kwa kishindo na jambo lililo mbele yao hivi sasa ni kuhakikisha wanajenga uwanja wa kuchezea mechi na mazoezi utakaojengwa kisasa utakuwa na hostel, mabwawa ya kuogelea.
“Ninaamini hiyo itasaidia kupunguza gharama za hotel tunazozitumia katika kupanga wakati timu ikiingia kambini kujiandaa na michezo yetu ya ligi na mashindano mengine,” alisema Nugaz.
Stori na Wilbert Molandi, Dar es salaam
