

“Wakati tunaingia madarakani, nchi yetu ilikuwa na vijiji 3,000 tu vilivyokuwa na umeme lakini sasa vimefika 9,402 na tumebakisha vijiji kama 3,000 kumaliza vyote. Sasa tukipewa miaka mitano tena kwa nini tushindwe kumaliza vijiji hivyo? Ndugai nitashangaa sana kama nunge lijalo hawatokupa uspika tena. Najua watasema nakupigia kampeni lakini ndiyo ukweli unachapa kazi vizuri. Ulisimama kidete kusimamia sheria ambazo zimesaidia kulinda rasilimali zetu.
“Nilipoiona Dodoma ilivyo nilijiuliza nikiwa njiani, nikasema Dodoma kweli imekuwa hivi, mbona sikuikuta hivi nilipoteuliwa kuwa rais? Nikafurahi nikaona ndoto za Baba wa Taifa zimekamilika kwamba Dodoma ni makao makuu ya nchi yetu.

“Tanzania ni taifa tajiri, lakini tulikuwa tumezoeshwa kuambiwa ni maskini na ndiyo maana Tanzania imeingia uchumi wa kati. Afrika nchi chache zimeingia uchumi wa kati ni Tanzania, Nigeria, Afrika Kusini, Kenya, Togo. Nataka Tanzania iwe kama Ulaya, nataka nchi hii iwe kama Ulaya, sisi ndiyo tuwe tunatoa misaada na uwezo tunao na kikubwa ni mipango na mipango imetengezwa na Chama changu cha Mapinduzi.”
“Tumechoka taifa hili unalima pamba unaisafirisha kama malighafi, halafu wakishatengeneza nguo wanazivaa wanakuletea mitumba wakati pamba ni yako. Sisi tunataka tukilima pamba tunaichakata hapa, zile nguo tunawapelekea ikiwezekana tunazivaa kwanza.
“Nataka korosho tuzivune na kuziongezea thamani Tanzania. Malighafi zitumike kwenye mambo mengine, kisha tunazisafirisha kwenda kuuza. Tuvae viatu kutoka viwanda vyetu. Kwenye madini tumechezewa sana yalisemwa mengi, nilisimama kusema bora kufa ukiwa unaitetea nchi.

“Mtu akisema nitapigiwa kura na vituo vya afya najua ndiyo wameshaanza kunipigia kampeni hivyo, maana vituo vya afya wametibiwa wanawake watanipigia kura. Wazee hata walevi walilala humo watanipigia na inanipa nguvu kuwa ushindi wa mwaka huu utakuwa mkubwa.
“Ninaogopa kwamba hao ukiwaachia inawezekana hizi meli zitapigwa mnada, inawezekana dhahabu hizi zitakuwa zinachimbwa wanauziana wao, ndiyo maana nimeguswa ndugu zangu, miaka mitano mingine niendelee kufanya kazi kwa sababu mambo ni mengi,” alisisitiza.