JESHI la polisi mkoani Pwani, linawashikilia wahamiaji haramu (wanaume) kutoka nchini Ethiopia wapatao 51, kwa kosa la kuingia nchini bila kibali.
Kamanda wa polisi mkoani humo,Wankyo Nyigesa, alithibitisha juu ya tukio hilo ambapo alisema huko eneo la Mzani wa magari Msata, Chalinze, polisi wakiwa doria barabara kuu ya Chalinze kuelekea Tanga, walikamata gari namba T 246 BBG aina ya Ccania tani 10, Hard Top.
Alisema gari hilo lilipopekuliwa lilikutwa likiwa na raia 51 wote wanaume wanaokadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 15-25 ambao walikuwa wanasafirishwa kutoka Tanga kuelekea Chalinze kupitia Msata na watu wawili wanaodhaniwa kuwa WaTanzania ambao walitoka ndani ya gari na kukimbia.
Wankyo alibainisha gari hilo linaonyesha linamililiwa na Uswege Mwamboma wa Tukuyu, Mbeya. Kamanda huyo aliwataka mmiliki wa gari na ambao wamehusika kuwasafirisha wahamiaji hao haramu kujisalimisha wenyewe kabla hawajatiwa nguvuni.
