MGOMBEA mwenza wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Salum Mwalimu, amesema iwapo chama hicho kitaingia madarakani kitahakikisha watu wa mkoa wa Tabora wanarudishiwa kilimo cha zao la pamba na kuhakikishiwa upatikanaji wa soko la zao hilo.
Ameyasema hayo jana Septemba 20, 2020, wakati akinadi sera za chama hicho katika mkoa huo ambapo pia amewaahidi watu wa Tabora upatikanaji wa maji safi, elimu bora pamoja na masoko ya mazao ya tumbaku na pamba.
“Watu wa Tabora Kaskazini mkituchagua tutahakikisha tunawarudishia zao lenu la pamba na tutahakikisha pamba yenu mtaweza kuuza sehemu kwa yeyote mnayemtaka sio kwenye vyama vya ushirika vinavyowakopa pamba yenu,’’alisema na kuongeza:
“Hiki ni kipindi cha kupanga upatikanaji wa elimu bora, upatikanaji wa maji safi, soko la tumbaku yetu na upatikanaji wa soko la pamba yetu.’’
Aidha, amesema kwa sasa chama hicho ndicho chenye ilani bora ambapo amewaomba wananchi kukichagua ili waweze kuleta mageuzi ya kiutawala, kiuchumi na kijamii.
