×

Mtoto Afariki Tumboni Baada ya Mume Kumkata Mkewe Tumbo

POLISI nchini India wanasema mwanamke mjamzito ambaye anadaiwa kukatwa tumbo na mume wake amezaa mtoto wa kiume aliyefariki akiwa tumboni. Familia ya mwanamke huyo inadai kuwa mume huyo alimshambulia akitaka kujua jinsia ya mtoto.

 

Wanasema wanandoa hao wana watoto watano wa kike na kwamba mwanamume huyo amekuwa akimhangaisha mke wake amzalie mtoto wa kiume. Mwanamume huyo ambaye tayari amekamatwa amekanusha madai ya kumshambulia makusudi mke wake akisema ilikuwa ni ajali.

 

Kisa hicho kilitokea katika wilaya ya Badaun, Uttar Pradesh, jimbo la India lililo na watu wengi zaidi Kaskazini mwa nchi hiyo ambapo mwanamke aliyejeruhiwa anaendelea kupokea matibabu na kwamba hali yake imeimarika katika Hospitali ya mji mkuu wa Delhi.

 

Kwa mujibu wa ndugu yake, mwanamke huyo alipelekwa Delhi siku ya Jumapili kufuatia ushauri wa daktari kwa sababu hali yake ilikuwa mbaya sana. Mume wake aliviambia vyombo vya habari nchini humo kuwa alimrushia upanga lakini hakujua itamuuimiza vibaya hivyo lakini polisi wanaendelea na uchunguzi zaidi.

 

“Nina watoto watano wa kike, mwanangu mmoja wa kiume amefariki. Najua watoto ni zawadi kutoka kwa Mungu. Sasa chochote kitakachotokea, kitatokea,” alisema.

 

Shauku ya baadhi ya wazazi nchini India kupata watoto wa kiume badala ya watoto wa kike imefanya watoto wengi wa kike kuuawa kabla ama baada ya kuzaliwa. Wasichana milioni 46 walitoweka India katika kipindi cha miaka 50, kwa mujibu wa ripoti ya mwezi Juni ya mfuko wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalosimamia idadi ya watu (UNFPA).

 

Kila mwaka, watoto wa kike karibu 460,000 wanauawa kupitia utoaji mimba huku vifo vingi vya watoto wa kike wanaozaliwa na kutelekezwa baada ya kuzaliwa vikiripotiwa.

 

Mwaka 2018 ripoti ya serikali ya India ilisema hamu ya kutaka watoto wa kiume imechangia kuzaliwa kwa watoto milioni 21 wa kike ambao “hawatakikani”. Ripoti hiyo ya Wizara ya Fedha ilibaini kuwa wanandoa wengi wanaendelea kuzaa hadi wapate mtoto wa kiume.

Leave a Comment