MKUU wa Mkoa Dar es Saalam, Abubakari Kunenge, leo Septemba 30, 2020, amefanya ziara ya ukaguzi katika eneo la Daraja la Kigamboni ambapo panajengwa.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo aliyoambatana na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dar es Salaam, SCP Lazaro Mambosasa, Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Sara Msafiri, na viongozi waandamizi wa mkoa huo amesema:
“Eneo hili lenye urefu wa kilomita mbili, palikuwa na mgogoro, na Mheshimiwa Rais Magufuli aliagiza pashughulikiwe. Tunashukuru mgogoro huo umemalizika na pamejengwa vizuri na kukamilika ndani ya muda wa mkataba na kwa gharama zilizotakiwa.
“Mheshimiwa Rais amesisitiza kuboresha miundombinu katika maeneo yetu, anatamani Tanzania iwe kama Ulaya, na eneo hili ambalo lipo Kigamboni patakuwa pazuri kama Ulaya na pengine hata zaidi ya Ulaya. Naona tayari mmeshaanza kupanda nyasi, tunataka Dar es Salaam iwe ya kijani. Nafahamu tuna maeneo mengi ya utalii.
“Wananchi wa Kigamboni mhakikishe suala la ulinzi linazingatiwa, kumbukeni taabu mliyokuwa mkiipata hapa kabla ya daraja hili kujengwa, hivyo tutunze miundombinu hii tusiiharibu,” amesema Kunenge.
