
Bodi ya Filamu nchini leo imemkutanisha mmilikiwa kituo cha luninga ya mtandaoni ya Nuella TV, Bwana Charles Liburd kutoka nchini Uholanzi na wadau wa filamu nchini ambapo amewaelezea nia yake ya kununua filamu za wasanii wa hapa nchini na kuzitumia kwenye luninga yake hiyo.
Akizungumza kwenye mkutano huo uliofanyika Uwanja wa Benjamini Mkapa Jijini Dar, Kaimu Mkurugenzi wa Bodi ya Filamu nchini, Dkt. Kiango Kilonzo amesema Bwana Liburd ameletwa hapa nchini na serikali ya Tanzania baada ya kuuchunguza mpango wake na kubaini jinsi unavyoweza kuwaingiza wadau wa filamu hapa nchini katika soko la kimataifa na kuwainua kiuchumi.

Dkt. Kilonzo amewataka wadau waliohudhuria mkutano huo kuacha kuufananisha mpango huo na baadhi ya watu waliowahi kuja hapa nchini na kujifanya kuisaidia tasnia ya filamu na baadae kuwaacha kwenye mataa.
“Naomba mnielewe vizuri, msije mkaufananisha mpango na mipango mingine kama hii iliyowahi kupita na kuacha lawama, hiyo haikuwa mipango ya serikali lakini mpango wa Bwana Liburd unasimamiwa na serikali kupitia bodi ya filamu.” Alimaliza kusema Dkt. Kilonzo.

Naye Bwana Liburd amesema kinachotakiwa ni mtu mwenye filamu yenye ubora kutuma filamu yake kwenye luninga hiyo ambapo ikifanikiwa kuingizwa kwenye mpango huo mmiliki atapata asilimia 50% ya mapato hayo kulingana na watazamaji (viewers) wake ambao watakuwa wakionekana kidijitali.

Liburd amesema hata kama filamu hiyo itakuwa imeshaingizwa kwenye mitandao mingine kama vile Youtube bado haiwazuii kupeleka na kwenye chanel yake. Alisema Liburd.