×

Kocha Barca Atarajia Miujiza Dhidi ya PSG

KOCHA wa Barcelona, Ronald Koeman, alifurahi kuona timu yake ikitoka nyuma na kuichapa Sevilla kisha ikatinga fainali ya Copa del Rey, lakini akasisitiza mechi dhidi ya Paris Saint-Germain kesho Jumatano itakuwa ni tofauti.

 

Barcelona waliingia katika mchezo wa nusu fainali ya Copa del Rey Jumatano iliyopita kwenye Uwanja wa Camp Nou, wakiwa nyuma kwa mabao 2-0, lakini walipambana na kupata mabao kutoka kwa Ousmane Dembele na bao la sekunde ya mwisho la Gerard Pique ambalo liliipeleka mechi kwenye muda wa ziada.

 

 

Kisha Martin Braithwaite akafunga katika kipindi cha kwanza cha muda wa ziada na kufanya Barca isonge mbele kwa jumla ya mabao 3-2. Ushindi huo umewafanya Barca waamini kuwa wanaweza kufanya maajabu pia dhidi ya PSG ambao wanaongoza dhidi yao 4-1.

 

 

Katika mchezo wa kwanza wa hatua ya 16 bora ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya PSG, Barca walichapwa 4-1 nyumbani, na sasa wana mlima mrefu wa kupanda ili kupindua matokeo ugenini Jumatano.Lakini Koeman amesema: “Ni rahisi kupindua matokeo ya 2-0, kuliko ya 1-4.

 

 

PSG wana timu nzuri na wachezaji bora. Tutaanza mechi kwa lengo la ushindi, kuona kama kuna nafasi ya kusonga mbele. Ninajivunia timu yangu. Kweli, siwezi kuomba zaidi ya kile walichokitoa.”

Leave a Comment