

Serikali kupitia Wizara Ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeanzisha oparesheni maalumu ya ufatiliaji wa wadaiwa wa Kodi ya Ardhi na viwanja ili kuwakumbusha wananchi kulipia ardhi zao kwa wakati kuepusha usumbufu na malimbikizo ya madeni serikalini.
Akizungumza na global Tv Kamishina wa Ardhi msaidizi Mkoa wa Dar es Salaam Bw. Idrisa Kaera amesema, wameamua kuanzisha mkakati huo ili kuwafikia wananchi wote wanaodaiwa Kodi ya Ardhi waweze kulipa madai yao ili kuiwezesha wizara na Serikali kutekeleza miradi yake kwa wakati.

Kamishina Kayera pia amewasihi wananchi kuwapa ushirikiano vijana hao katika kutimiza majukumu yao kwakua wanafanya kazi hiyo kwa mjibu wa Sheria na taratibu za wizara, vivyo hivyo ametoa wito kwa wadaiwa wote wa Ardhi kulipa Kodi kwa wakati bila kusubiri kusukumwa na mamlaka husika.
Oparesheni hiyo inafanywa na vijana waliopewa mafunzo na vitambulisho maalumu na watapita nyumba kwa nyumba kuwapa wateja maelekezo na elimu ya namna ya kulipa Kodi zao kwa urahisi zaidi kwa mfumo wa kidijitali yaani kupitia simu zao za mkononi au mawakala wa taasisi za kifedha.
Zoezi hilo linalotarajiwa kufanyika kwa siku 14 katka wilaya zote za mkoa wa Dar es Salaam na limelenga kuwakumbusha na kutoa elimu zaidi ya umuhim wa kulipa Kodi ya Ardhi kwa wakati ili kufanikisha mipango ya maendeleo ya Serikali.