
JIWE kubwa zaidi duniani la madini ya ruby kutoka nchini Tanzania, limegeuka na kuwa gumzo kubwa Dubai, Falme za Kiarabu ambapo kwa mara ya kwanza limewekwa hadharani na kutoa fursa kwa watu kulitazama na kupiga nalo picha.
Jiwe hilo la madini ya ruby lina uzito wa kilogram 2.8 sawa na carat 8400 na linatarajiwa kupigwa mnada kwa dola za Kimarekani Milioni 120 ambapo limeweka rekodi duniani kote kuwa jiwe kubwa zaidi la ruby ghafi kuwahi kupatikana.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Burji el Hama ambao ndiyo wamiliki wa madini hayo, wamesema watu wengi wamekuwa wagumu kuamini kama kuna madini ya ruby yenye ukubwa kama huo kwa hiyo wameamua kuliweka jiwe hilo kwenye maonesho ya halaiki ili kila mtu ajionee na baada ya muda, wataanza kulizungusha sehemu mbalimbali ili wale wasioamini, nao wapate nafasi ya kujionea kwa macho yao.
Amesisitiza kwamba jiwe hilo ni la madini ghafi ya ruby yakiwa hayajasafishwa wala kuchakatwa, jambo linaloyafanya kuwa ya kipekee zaidi kwa sababu hakujawahi kupatikana jiwe kubwa kama hilo kutoka mahali pengine popote duniani zaidi ya Tanzania.