×

Watu 6 wa Familia Moja Mkoani Songwe Wanasakwa na Polisi kwa Uharibifu wa Mazingira

Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Omary Mgumba

MKUU wa Mkoa wa Songwe, Omary Mgumba amemuagiza Kamanda wa Jeshi la Polisi kuwatafuta popote pale walipo watu sita (6) ambao wanatuhumiwa kwa kuhatarisha amani na uharibifu wa mazingira katika msitu wa Namwangwa uliopo Kijiji cha Namwangwa Kata ya Hezya Wilaya ya Mbozi.

 

Mkuu wa Mkoa amechukua hatua hiyo Juni 1 wakati wa ziara yake baada ya kujionea uharibifu wa mazingira uliofanyika katika msitu wa Namwangwa alipokuta miti imekatwa hovyo na uwepo matanuri ya mkaa pembezoni mwa msitu huo.

 

Watuhumiwa wanaotafutwa ni Eliud Shizya Mwashilindi, Rashid Charles Mwashilindi, Rasco Wiliad Mwashilindi, Michael Pondamali Msukwa, Rapheel Alnasi Mwambala na Yona Watson Mwambala.

 

Waarifu hao wa Mazingira walitaka kuwateka waandishi wa Habari pamoja na kumkamata na kumteka mtumishi mmoja na kushinikiza wamuachie mwenzao aliyekamatwa ndipo watumishi kwa hofu ya maisha ya mwenzao wakamuachia yule muarifu.

 

Mkuu wa Mkoa amesema Serikali haiwezi kuwaacha waarifu watambe na mazingira yanaharibika na kuonyesha kama wanaweza kufanya kitu chochote ni lazima tuonyeshe Serikali ipo, inafanya kazi, ina meno na haijashindwa kitu chochote.

 

“Nimeisha piga marufuku kuchoma mkaa na kukata miti ovyo lakini kitendo kinachofanyika katika msitu wa Namwanga ni kama vile hakuna zuio la aina yeyote hakuna Serikali” Omary Mgumba.

 

Mkuu wa Mkoa amemuagiza Kamanda wa Jeshi la Polisi Songwe kuwafungilia kesi za kutishia kuua, uhujumu uchumi, waharibifu wa mazingira pamoja na kuua baadhi ya mifugo ya mwananchi.

 

Mkuu huyo wa Mkoa amesema watuhumiwa hao sita ndio mwanzo wa kazi ambayo imeanza ya kukomesha uharibu wa mazingira katika msitu wa Namwangwa.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe amesema watu hao 6 watakuwa mfano kwa wengine

“kwa vitendo hivi vilivyotokea na hali niliyoiona ile ya Uharibifu wa mazingira lazima Serikali ichukue hatua kwa kuwakamata watu wote vinara, viongozi ili watusaidie Serikali.

 

Pia, Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Omary Mgumba amemuagiza Katibu Tawala Mkoa wa Songwe kuwasimamisha kazi watendaji wa vijiji vinavyozunguka msitu wa Namwangwa, Mtendaji wa Kata ya Hezya, Afisa Tarafa wa Vwawa, Afisa Misitu wa Halmashauri na Afisa Mazingira wa Halmashauri ya Mbozi.

 

Katika hatua nyingine amemuagiza Katibu Tawala wa Mkoa kuunda haraka Kamati maalumu ya kuwachunguza watumishi wote waliosimamishwa ili kujua kwa nini hali hii imetokea amesema Mhe. Omary Mgumba.

 

“Kwa hali niliyoikuta ya uharibifu wa mazingira ni mbaya sana na kama Rais angekuja leo hapa mie ningechukulia hatua sasa siwezi kuacha hali hii iendelee” Mhe. Omary Mgumba.

 

Aidha, Mkuu wa Mkoa amemuagiza Kamanda wa Jeshi la Polisi Songwe kuwakamata wenyeviti wa vijiji na vitongoji vinavyozunguka msitu wa Namwanga kwa ajili ya kuisadia Serikali kuwapata watu wote wanaoharibu mazingira msitu wa Namwanga.

 

Wakati huo huo Mkuu wa Mkoa ametoa wito kwa wananchi kutoa ushirikiano kwa Serikali wa siri na Serikali itatunza Siri iyo.

Leave a Comment