
MSHAMBULIAJI wa Klabu ya Real Madrid, Karim Mostafa Benzema ana majeraha katika kidole cha mwisho cha kulia chake kwa takribani miaka mitatu sasa tangu Januari mwa mwaka 2019 wakati wa mechi yao dhidi ya Real Betis.
Benzema, 34, ambaye pia ni mshambuliaji wa Timu ya Taifa ya Ufaransa alikataa kufanyiwa upasuaji kwenye kidole hicho kwa sababu upasuaji huo ungemfanya akae nje ya uwanja kwa miezi miwili, kwa mujibu wa daktari wa klabu ya Real Madrid.

Lakini Karim ambaye asili yake ni Algeria, baada ya kuambiwa atakaa nje miezi miwili aliamua kukataa kufanyiwa upasuaji huo ili aendelee kusakata kabumbu na kuitumikia klabu yake ambayo msimu uliopita aliisaidia kuchukua Ubingwa wa La Liga na UEFA Champions League pamoja na mataji mengine.
Ari hiyo ya kupambana ndiyo imempa mafanikio makubwa Mfaransa huyo na kufanikiwa kutwaa Tuzo ya Ballon d’Or hivi karibuni akiwa amefunga mabao 44 katika mechi 46 alizocheza yakiwemo mabao 15 kwenye Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya.