
RAIS wa Iran, Ibrahim Raisi ameapa kulipiza kisasi dhidi ya kundi la kigaidi lililotekeleza mashambulizi katika sehemu ya ibada ya waumini wa Shia na kusababisha vifo vya watu 15.
Pia, watu 19 walijeruhiwa kwenye shambulizi hilo lililotekelezwa wakati wa ibada ya jioni kwenye eneo la makaburi la Shah Cheragh katika Jiji la Shiraz.
Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Rais, imelaani vikali aliyowaita maadui wa Iran wanaojaribu kuligawa taifa hilo kwa kutumia machafuko na ugaidi.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Hossein Amirabdollahian ametoa onyo kuwa serikali haitaruhusu usalama na maslahi ya Iran kuchezewa na aliowataja kuwa magaidi na wavamizi wa kigeni wanaodai kutetea demokrasia.

Kamanda wa kikosi maalum cha kijeshi cha Iran, Hossein Salami amesema kwamba moto wa kulipiza kisasi utawafikia waliotekeleza shambulizi hilo.
Maafisa wa Iran wamesema kwamba wamemkamata mtu aliyekuwa na bunduki ambaye anadaiwa kutekeleza shambuliio hilo katika sehemu takatifu ya kuabudu ya Cheragh, iliyopo katika Mji wa Shiraz nchini humo.
Mauaji hayo ya mahujaji wa Washia, yamefanyika siku ambayo maafisa wa usalama wa Iran wakikabiliana na waandamanaji waliojitokeza kuadhimisha siku 40 za kifo cha Amini.

Shambulio hilo linaongeza shinkizo dhidi ya serikali inayokabiliwa na maandamano kutoka sehemu mbalimbali nchini humo kutokana na kifo cha Mahsa Amini mwanamke mwenye umri wa miaka 22 mwenye asili ya kikurdi, aliyefariki dunia akiwa mikononi mwa polisi, Septemba 16, mwaka huu.
Kundi la kutetea haki za kibinadamu la Hengaw limesema kwamba vijana wawili walipigwa risasi na kuuawa wakati wa maandamano hayo yaliyofanyika katika Mji Mkuu wa Mkoa wa Kurdistan, Sanandaj.
Imeandaliwa na Sanifa Khalifa kwa msaada wa mtandao