×

Waliopata Division one St. Anne Marie Academy, Kutembelea Mbuga za Wanyama

Mkuu wa shule ya St Anne Marie Academy ya Mbezi Kimara kwa Msuguri, Gladius Ndyetabula, akimpa zawadi ya vitabu mmoja wa wahitimu wa kidato cha nne wa shule hiyo

WANAFUNZI wa shule ya St. Anne Marie Academy waliofanya vizuri kwenye matokeo ya kidato cha nne wanaandaliwa ziara ya kutembelea mbuga za wanyama za Mikumi na Ngorongoro kama motisha ya kuwafanya wengine nao wafanye vizuri.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa shule hiyo, Gladius Ndyetabura wakati akizungumza kuhusu matokeo ya kidato cha nne ambapo wanafunzi 103 wa shule hiyo walifanikiwa kupata daraja la kwanza.

Amesema kwenye mtihani huo wanafunzi 40 walipata daraja la pili na wanafunzi saba pekee ndio wamepata daraja la tatu.

“Haya ni matokeo mazuri sana kwetu ukizingatia tulikuwa na wanafunzi wengi lakini wote wamefanikiwa kupata nafasi ya kuendelea na kidato cha tano ndiyo maana tunawaandalia safari hii ya kwenda Mikumi na Ngorongoro kama motisha kwao na kwa wenzao ili wapate ari ya kufanya vizuri,” alisema

Mkuu wa shule ya St Anne Marie Academy ya Mbezi Kimara kwa Msuguri, Gladius Ndyetabula, akimpa zawadi ya ngao mmoja wa wahitimu wa kidato cha nne wa shule hiyo ambayo kwenye matokeo hayo wanafunzi 103 wa shule hiyo wamepata daraja la kwanza na 40 daraja la pili na saba kupata daraja la tatu.

Aliwapongeza na kuwashukuru walimu wa shule hiyo ambao wamefanya kazi kubwa usiku na mchana kuhakikisha wanafunzi wote wanafaulu kwa ufaulu wa  juu na alimshukuru pia Mkurugenzi wa shule hiyo, Dk. Jasson Rweikiza kwa ushirikiano ambao amekuwa akiutoa kwa walimu.

Alitaja siri ya mafanikio hayo kuwa ni shule kuwa na mazingira mazuri ya wanafunzi kusoma ikiwemo maktaba ya kisasa  na maabara iliyosheheni vifaa vya kutosha pamoja na walimu mahiri wanaojua kazi yao

“Wanafunzi wetu wanakula milo minne kwa siku na tuna mashamba ya mboga mboga na matunda kwa hiyo wanakula mlo kamili na mazingira kwa ujumla ni mazuri sana kuwawezesha kujisomea muda wowote,” alisema

Alisema shule hiyo imedhibiti ulinzi kwa kuweka walinzi 46  wenye mafunzo wakisaidiwa na mbwa wao ambao wamekuwa wakizunguka usiku na mchana kuhakikisha kunakuwa na usalama.

Wahitimu wa shule ya St Anne Marie Academy ya Mbezi Kimara kwa Msuguri jijini Dar es Salaam wakiwa kwenye picha na Mkuu wa shule hiyo, Gladius Ndyetabula.

“Hawa walinzi wetu wamepata mafunzo ya kisasa kiasi kwamba hata ukitokea moto wakotayari kuuzima ndani ya dakika chache kwa hiyo wazazi msiwe na wasiwasi kuhusu taaluma na suala la usalama,” alisema

Mwaka 2021 St Anne Marie Academy ilitoa mwanafunzi bora kitaifa, Elulei Haule anayesoma kidato cha kwanza shule ya Marian Boys ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani.

Akizungumza kwenye mahafali ya kidato cha nne mwaka huu, Mkurugenzi wa shule hiyo, Dk. Rweikiza, alitangaza kwamba hakuna mwanafunzi yoyote wa shule hiyo atakayefukuzwa kwasababu ya kufiwa na wazazi wake na kukosa ada.

Alisema wakati wa mlipuko wa korona mtandao wa shule zake ulipoteza wazazi 46 lakini hakuna aliyewahi kufukuzwa kwa kushindwa kulipa ada na wanaendelea.

Wakiwa na furaha baada ya kuahidiwa kupelekwa mbuga za mikumi na Serengeti

“Nilisema wakati ule tulipopoteza wazazi 46 na narudia leo kusisitiza kwamba msimamo bado ni ule ule. Hata baada ya korona watu bado wanakufa kwasababu hakuna anayejua kesho yake,” alisema na kuongeza.

“ Kama mwanafunzi yuko shule ya msingi atamaliza darasa la saba bila kulipa ada na kama yuko sekondari atamaliza kidato cha nne bila kulipa ada

 

Leave a Comment