
Wanawake wilayani Mufindi wameiomba serikali kuwapa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri ili waweze kujiendeleza katika biashara zao na kujiinua kiuchumi na kuacha kukopa mikopo umiza.
Wanawake hao wamesema hayo leo mbele ya Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo na kueleza kuwa wamekuwa hawapati mikopo hiyo na badala yake wanakopa mikopo ya kausha damu na kuwafanya kushindwa kurejesha mikopo hiyo na kuishia kutelekeza familia na kukimbia madeni.

Mwajuma Mbata, Mjumbe wa CCM shina namba 3 Kata ya Boma, amesema mikopo hiyo inatolewa kwa masharti ya kutengeneza vikundi katika makundi maalum ya wajasiriamali wadogo lakini wanaopata mikopo hiyo ni wale wenye uwezo wa kukopa benki.
“Kukosekana kwa mikopo hiyo kunatufanya tunajiingiza katika mikopo ya moto, maarufu kama kausha damu na tukishindwa kulipa tunaachika katika ndoa zetu na kutelekeza watoto,” alisema na kuongeza kuwa wanaopata mikopo hiyo ni wale ambao wanauwezo wa kukopa katika mabenki na ndiyo baadaye wanalazimika kuomba mikopo kausha damu kwao ambayo inawaumiza.
“Tunaiomba serikali ituangalie na sisi wajasiriamali wadogo watupunguzie masharti hasa katika dhamana ili tunapojiunga katika vikundi hivyo tuweze kuipata mikopo hiyo na kujiinua kiuchumi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Chongolo, amesema kuwa serikali ilifanya maamuzi ya kusitisha mikopo ili kutengeneza utaratibu mzuri ambapo lengo lake ni kuwawezesha vijana walemavu na akina mama kujikwamua kiuchumi.
Amesema utaratibu huo utakuwa umekamilika mwezi wa 8 ambao utakuwa na tija kubwa kwa vijana na utakuwa na faida ya kiuchumi.
“Natoa wito kwa wananachi wote, vijana akina mama na walemavu kuwa ukikopa rejesha ili na wengine wakope, hii itaepusha kujiingiza katika mikopo ya kuumiza na kuwafanya kutelekeza familia na kuvuruga ndoa na usichukue mkopo kwa ajili ya kuolea wala kutoa mahari hivyo mikopo itakayotolewa itatatua changamoto ya mikopo umiza na kuleta tija katika familia.”