
RAIS Samia Suluhu Hassan amefanya mabadiliko ya baadhi ya viongozi ambapo aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Ahmed Abbas amehamishwa kutoka mkoa huo na kuwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma.
Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Rais Ikulu imeeleza Rais Samia pia amemhamisha Halima Omar Dendego kutoka Mkoa wa Iringa kwenda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Singida.

Aidha, Peter Joseph Serukamba amehamishwa kutoka Mkoa wa Singida kwenda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa.
Wakati huohuo, Batilda Salha Burian amehamishwa kutoka Mkoa wa Tabora kwenda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Tanga.
Wakuu wa Mikoa walioachwa kufuatia uteuzi na uhamisho wa viongozi mbalimbali uliofanywa leo Machi 09, 2024 na Rais Samia Suluhu Hassan ni Kanali Laban Thomas aliyekuwa Mkuu wa mkoa wa Ruvuma na Dkt. Francis Michael aliyekuwa Mkuu wa mkoa wa Mkoa wa Songwe.
