
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Novemba 20, 2024 amefika Kariakoo Jijini Dar es salaam muda mfupi baada ya kurejea kutoka Brazil, ambapo amekagua shughuli za uokoaji na kisha kuongea na Wananchi na kuthibitisha kuwa hadi kufikia asubuhi leo Watu 20 wamefariki kutokana na maafa ya ghorofa kuporomoka.

“Jitihada zetu kubwa katika tukio hili imekuwa kuwaokoa wenzetu walionasa katika jengo lile wakiwa hai lakini kama tunavyoambiwa jitihada haziondoshi kudra ya Mungu, pamoja na jitihada tulizofanya kuna wenzetu tumewapoteza” amesema Dkt. Samia.
“Taarifa niliyopewa leo kwamba mpaka saa tatu asubuhi tumepoteza wenzetu 20 ambao Serikali imeshirikiana na Familia kuwasitiri wenzetu”
“Hili sio pigo kwa Familia zilizopoteza Watu wao pekee yao ni pigo letu kama Watanzania na tunaguswa pia na kumbukumbu ya kutisha kwa wenzetu waliookoka hapa, kwa jinsi jengo lilivyo Mtu akitoka hai bila shaka hawapo sawa (kisaikolojia), niombe wasifadhaike, wajipe moyo na tuendelee na shughuli zetu za kawaida bado Mungu ana kazi nao.”



