×

Wabunge wa Marekani Wambana Waziri wa Ulinzi Kuhusu Vita dhidi ya Iran na Bajeti ya Jeshi – Video

Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth

Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth, anatarajiwa kukabiliwa na siku ya pili ya maswali makali kutoka kwa wabunge, hasa chama cha Democratic, kuhusu namna alivyoshughulikia vita dhidi ya Iran.

Katika kikao cha kwanza kilichodumu kwa karibu saa sita, wabunge walimuhoji kuhusu gharama kubwa ya vita hiyo, ambayo imefikia dola bilioni 25, pamoja na kupungua kwa silaha muhimu za kijeshi. Hata hivyo, Hegseth hakutoa majibu ya wazi kuhusu vita hiyo itaendelea kwa muda gani au itagharimu kiasi gani zaidi.

Kikao cha leo katika Kamati ya Seneti kinatarajiwa kuangazia pia pendekezo la bajeti ya ulinzi ya mwaka 2027, ambalo linafikia dola trilioni 1.5 kiwango kikubwa zaidi kuwahi kupendekezwa. Hegseth pamoja na viongozi wa jeshi wataeleza umuhimu wa kuongeza uwekezaji katika ndege zisizo na rubani, mifumo ya ulinzi wa makombora na meli za kivita.

Wabunge wa Democratic wanatarajiwa kuendelea kuhoji mkakati wa vita hiyo, ambayo kwa sasa ipo katika makubaliano dhaifu ya kusitisha mapigano, pamoja na uamuzi wa Hegseth kuwafukuza baadhi ya maafisa wa juu wa jeshi. Wakati huo huo, wabunge wa Republican wanaonekana kuunga mkono operesheni hiyo huku wakijikita zaidi katika masuala ya bajeti ya kijeshi.

Maswali mengine yanahusu shambulio lililosababisha vifo vya zaidi ya watu 165, wakiwemo watoto, baada ya shule moja nchini Iran kushambuliwa. Tukio hilo bado linafanyiwa uchunguzi huku taarifa zikionyesha uwezekano wa kuhusika kwa Marekani.

Aidha, Hegseth alikabiliwa na maswali kuhusu kifo cha wanajeshi sita wa Marekani waliouawa kwa shambulio la ndege isiyo na rubani nchini Kuwait, lakini hakutoa jibu la moja kwa moja kuhusu kama tukio hilo lingeweza kuzuilika.

Katika hoja nyingine tata, Hegseth alidai kuwa miundombinu ya nyuklia ya Iran iliharibiwa kabisa katika mashambulizi ya awali. Kauli hiyo ilipingwa na baadhi ya wabunge waliouliza kwa nini vita ilianzishwa ikiwa tishio hilo lilikuwa tayari limeondolewa.

Leave a Comment