×

Rais Samia Kufanya Ziara ya Kihistoria Urusi Kukutana na Putin

Rais Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kufanya ziara ya kitaifa ya siku tatu nchini Russia kuanzia Jumatano Juni 3 hadi 5, 2026.

Katika ziara hiyo, Rais Samia atafanya mazungumzo rasmi na Rais wa Russia Vladimir Putin pamoja na kushiriki katika St. Petersburg International Economic Forum 2026 maarufu kama SPIEF.

Jukwaa hilo ni miongoni mwa mikutano mikubwa duniani inayowakutanisha wakuu wa nchi, viongozi wa biashara, wawekezaji, taasisi za fedha pamoja na wataalamu wa sera kujadili mwenendo wa uchumi wa dunia na fursa za ushirikiano wa kimataifa.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Bakari Machumu, ziara hiyo ni ya kihistoria kwani ni mara ya pili kwa Rais wa Tanzania kufanya ziara rasmi nchini Russia tangu ile ya Julius Nyerere mwaka 1969.

Aidha, Rais Samia anatarajiwa kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Uzamivu (Honoris Causa) na RUDN University kwa kutambua mchango wake katika uongozi, mageuzi ya elimu, kuimarisha diplomasia ya Tanzania pamoja na kuitangaza nchi kimataifa.

Leave a Comment