×

Trump Atangaza Makubaliano ya Kusitisha Mapigano kati ya Israel na Hezbollah

Serikali ya Lebanon imetangaza makubaliano ya usitishaji wa sehemu wa mapigano kati ya kundi la Hezbollah na Israel, hatua inayotajwa kuwa jaribio la kupunguza mvutano wa vita vilivyogharimu maelfu ya maisha.

Kwa mujibu wa ubalozi wa Lebanon mjini Marekani, makubaliano hayo hayatamaliza kabisa vita, bali yanaitaka Israel kusitisha mashambulizi dhidi ya mji wa Beirut na maeneo ya vitongoji vinavyodhibitiwa na Hezbollah, huku kundi hilo likiahidi kusitisha mashambulizi yake dhidi ya Israel.

Hata hivyo, mapigano yaliendelea kusini mwa Lebanon ambako jeshi la Israel limeendelea na operesheni zake za kijeshi. Jeshi la Israel lilisema mapema Jumanne kuwa lilidungua makombora mawili yaliyovuka kutoka Lebanon kuelekea kaskazini mwa Israel bila kusababisha majeruhi.

Rais wa Marekani Donald Trump ndiye aliyetangaza kwanza makubaliano hayo, akidai kuwa Hezbollah kupitia wapatanishi wake iliahidi kutoshambulia Israel. Pia alisema Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu alikubali kuondoa vikosi vilivyokuwa vikijiandaa kushambulia Beirut.

Baada ya tamko hilo, Netanyahu alisema Israel itaendelea na operesheni zake kusini mwa Lebanon, ambako vikosi vya ardhini vinaelekea katika Mto Zaharani, eneo linalotajwa kuwa hatua ya ndani zaidi ya jeshi hilo kuingia Lebanon katika kipindi cha miaka 25.

Mbunge wa Hezbollah Hassan Fadlallah alisema kundi hilo linaunga mkono usitishaji kamili wa mapigano nchini Lebanon kama hatua ya kwanza kuelekea kuondolewa kwa wanajeshi wa Israel.

Lebanon imesema inatarajia kupanua makubaliano hayo kupitia mazungumzo zaidi yatakayofanyika Washington Jumatano.

Wakati huo huo, Iran imeonya kuwa inaweza kusitisha mazungumzo yake yasiyo ya moja kwa moja na Marekani kuhusu amani kutokana na vita vinavyoendelea Lebanon. Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araqchi alisema usitishaji wa mapigano kati ya Iran na Marekani unapaswa kuhusisha pia Lebanon.

Aidha, kamanda wa kikosi cha Quds Force Esmaeil Qaani ametishia kupanua vizuizi vya usafiri wa majini kutoka Mlango wa Hormuz hadi Bab el-Mandeb, hatua inayoweza kuathiri biashara ya mafuta duniani.

Kutokana na hali hiyo, bei ya mafuta duniani ilipanda kwa asilimia 4 Jumatatu huku hofu ya kuongezeka kwa mvutano wa Mashariki ya Kati ikiendelea kuongezeka.

Leave a Comment