×

Iran Yalalamikia Vikwazo vya Visa Kabla ya Mechi ya Kombe la Dunia

Kocha wa timu ya taifa ya Iran, Amir Ghalenoei

Kocha wa timu ya taifa ya Iran, Amir Ghalenoei, amesema mvutano wa kisiasa pamoja na matatizo ya upatikanaji wa visa vimeathiri maandalizi ya timu yake kuelekea mchezo wa kwanza wa Kombe la Dunia 2026 dhidi ya New Zealand.

Iran imewasili kwenye mashindano hayo ikiwa katikati ya hali ya sintofahamu kufuatia uhusiano mbaya wa kidiplomasia kati ya Tehran na Washington, ambapo baadhi ya maafisa wa timu hiyo walikumbwa na changamoto za kupata visa vya kuingia Marekani.

Akizungumza kabla ya mchezo huo utakaopigwa jijini Los Angeles, Ghalenoei alisema timu yake haitaruhusu mazingira ya nje kuathiri malengo yao ya kisoka.

“Tupo hapa kucheza mpira wa miguu na kuwakilisha wananchi wa Iran. Hatutaki kujihusisha na mijadala ya kisiasa wala mambo yanayotokea nje ya uwanja,” alisema kocha huyo.

Iran inatarajiwa kucheza mechi yake ya ufunguzi dhidi ya New Zealand katika tukio linalotajwa kuwa la kipekee, likiwa ni mara ya kwanza kwa nchi mwenyeji wa Kombe la Dunia kuikaribisha timu kutoka taifa ambalo limekuwa kwenye mgogoro wa kijeshi nalo.

Licha ya kutangazwa kwa makubaliano ya amani kati ya Marekani na Iran saa chache kabla ya mchezo huo, hali ya tahadhari imeendelea kuonekana huku makundi ya Wairani wanaoishi nje ya nchi yakipanga maandamano nje ya uwanja kupinga serikali ya Tehran.

Nahodha wa safu ya ushambuliaji ya Iran, Mehdi Taremi, alisema mvutano huo unapunguza furaha ambayo mashindano ya soka yanapaswa kuleta kwa mashabiki duniani.

“Tumekuwa tukizungumza kuhusu soka kama chombo cha kuleta amani na umoja, lakini hali ya sasa imeathiri uzoefu huo kwa kiasi kikubwa,” alisema Taremi.

Iran pia ililazimika kubadilisha kambi yake ya maandalizi mara mbili kabla ya mashindano, ikihamishwa kutoka Marekani kwenda Mexico kutokana na mazingira yaliyokuwepo.

Kocha Ghalenoei amesisitiza kuwa licha ya changamoto hizo, wachezaji wake wana ari kubwa ya kufanya vizuri na kuonyesha uwezo wao katika mashindano hayo makubwa.

Iran ipo Kundi G pamoja na New Zealand, Belgium na Misri, huku ikisaka historia ya kufuzu hatua ya mtoano kwa mara ya kwanza katika historia ya ushiriki wake kwenye Kombe la Dunia.

Leave a Comment