×

Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance Awasili Uswisi Kufanya Mazungumzo na Iran

Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance

Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance, amewasili nchini Uswisi kwa mazungumzo muhimu ya amani kati ya Marekani na Iran, huku mvutano ukiongezeka kuhusu madai ya Iran kufunga tena njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani, Hormuz.

Mazungumzo hayo yanafanyika wakati Marekani na Iran zikiwa zimekubaliana kusitisha mapigano kwa siku 60 ili kutoa nafasi ya mazungumzo ya kutafuta suluhu ya kudumu baada ya vita vilivyodumu kwa karibu miezi minne.

Hata hivyo, hali imezidi kuwa tete baada ya Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Iran (IRGC) kutangaza kuwa limefunga Hormuz kutokana na kile ilichodai kuwa ni ukiukwaji wa makubaliano ya usitishaji mapigano nchini Lebanon.

Iran imeishutumu Marekani kwa kushindwa kuizuia Israel kuendelea na mashambulizi nchini Lebanon, ikisema makubaliano ya muda yalihitaji kusitishwa kwa mapigano katika maeneo yote ya mzozo.

Hata hivyo, Jeshi la Marekani limekanusha madai hayo na kueleza kuwa shughuli za usafirishaji Hormuz zinaendelea kama kawaida. Kwa mujibu wa Kamandi Kuu ya Marekani (CENTCOM), zaidi ya meli 55 za biashara zilipita katika njia hiyo siku ya Jumamosi, zikisafirisha zaidi ya mapipa milioni 17 ya mafuta kwenda masoko mbalimbali duniani.

Wakati mazungumzo yakitarajiwa kuendelea nchini Uswisi, pande zote mbili zinaonekana kutofautiana kuhusu utekelezaji wa makubaliano ya awali yaliyopatanishwa na Pakistan na kusainiwa na Rais wa Marekani Donald Trump pamoja na Rais wa Iran Masoud Pezeshkian.

Leave a Comment