×

Trump Ataka Makubaliano, Aonya Hatua za Kijeshi Dhidi ya Iran

Rais wa Marekani, Donald Trump.

Rais wa Marekani, Donald Trump, ameionya Iran kuwa Washington iko tayari ama kufikia makubaliano ya kidiplomasia au kuchukua hatua kali za kijeshi, akisisitiza kuwa Marekani haitasita ikiwa mazungumzo yatashindwa kuzaa matunda.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Ofisi ya Oval, Ikulu ya Marekani, Trump alisema bado anatamani suluhisho la kidiplomasia, lakini akaonya kuwa Marekani ina uwezo wa kuchukua hatua za haraka dhidi ya miundombinu muhimu ya Iran.

“Tutafikia makubaliano au tutamaliza kazi. Ningependelea makubaliano kwa sababu sitaki kuwaathiri watu milioni 91 wa Iran,” alisema Trump.

Kauli hiyo imekuja baada ya duru za mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja kati ya Marekani na Iran kumalizika wiki iliyopita bila mafanikio ya wazi kuhusu makubaliano ya kudumu ya amani.

Mazungumzo hayo yalifanyika wakati wa kipindi cha usitishaji mapigano cha siku 60, kilicholenga kutoa nafasi kwa juhudi za kidiplomasia kufuatia mashambulizi ya Marekani na Israel yaliyosababisha kuanza kwa mzozo huo.

Kauli ya Trump pia imefuatia mazishi ya aliyekuwa Kiongozi Mkuu wa Iran, Ali Khamenei, ambapo maelfu ya Wairani walijitokeza kuonyesha mshikamano na kuashiria kuwa taifa hilo linaendelea kuwa na msimamo imara licha ya vita na shinikizo la kimataifa.

Licha ya juhudi za Marekani kufufua mazungumzo kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran, bado hakuna mwafaka uliopatikana, huku mvutano kati ya mataifa hayo ukiendelea kuwa chanzo kikuu cha wasiwasi kwa usalama wa Mashariki ya Kati.

Leave a Comment