
UBELIGIJI leo Julai 7, 2026 imefuzu robo fainali Kombe la Dunia 2026 baada ya kuichapa Marekani mabao 4-1 katika mchezo wa hatua ya 16 bora uliochezwa mjini Seattle, na sasa itakutana na Hispania kuwania tiketi ya nusu fainali.
Nyota wa mchezo alikuwa Charles De Ketelaere aliyefunga mabao mawili na kutoa pasi moja ya bao, akiiongoza Ubelgiji kutumia makosa ya safu ya ulinzi ya Marekani kupata ushindi mkubwa.
Marekani ilianza kwa presha baada ya kuruhusiwa kucheza kwa mshambuliaji Folarin Balogun, ambaye adhabu yake ya kadi nyekundu ilisimamishwa.
Hata hivyo, makosa ya walinzi pamoja na uzembe wa kipa Matt Freese yaliigharimu timu hiyo.
Malik Tillman aliisawazishia Marekani kwa bao la mpira wa adhabu dakika ya 31, lakini sekunde 61 baadaye De Ketelaere aliirejeshea Ubelgiji uongozi.
Kipindi cha pili, Hans Vanaken alifunga bao la tatu baada ya Freese kufanya kosa mbele ya lango lake, kabla ya Romelu Lukaku, aliyeingia akitokea benchi, kufunga bao la nne katika dakika za nyongeza.
Habari mbaya kwa Marekani ni kuumia kwa nahodha wake Christian Pulisic, ambaye alitolewa nje kipindi cha pili baada ya kuumia mguu wa kulia.
Ushindi huo umeifanya Ubelgiji kufikisha michezo 18 mfululizo bila kupoteza na pia kuiondoa Marekani katika hatua ya 16 bora kwa mara ya pili ndani ya miaka 12.
Marekani nayo imeshindwa kutinga robo fainali ya Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2002.
Sasa Ubelgiji itakutana na Hispania katika robo fainali, huku mshindi wa pambano hilo akitarajiwa kukutana na mshindi kati ya France na Morocco kwenye hatua ya nusu fainali.