
HARARE, Zimbabwe: Rais wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa, amesaini kuwa sheria muswada unaomruhusu kuendelea kubaki madarakani hadi mwaka 2030, baada ya mabunge yote mawili ya nchi hiyo kuidhinisha mabadiliko hayo.
Msemaji wa serikali, Nick Mangwana, alithibitisha hatua hiyo kupitia ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa X, akisema sheria hiyo sasa imekamilika na kuanza kutumika.
“Imesainiwa, imethibitishwa na sasa ni sheria,” aliandika Mangwana huku akiambatanisha nakala ya sheria hiyo.
Marekebisho hayo yanaongeza muda wa utawala wa Mnangagwa kwa miaka miwili zaidi baada ya kumalizika kwa muhula wake wa pili wa urais mwaka 2028.
Mbali na kuongeza muda wa uongozi, sheria hiyo pia ina kipengele kinachobadilisha mfumo wa uchaguzi wa rais, ambapo inatoa uwezekano wa rais kuchaguliwa na Bunge badala ya kuchaguliwa moja kwa moja na wananchi kupitia kura.
Dalili kwamba Mnangagwa alikuwa akitaka kuendelea kuongoza Zimbabwe baada ya mwaka 2028 zilianza kuonekana miaka miwili iliyopita, baada ya baadhi ya wafuasi wake ndani ya chama tawala ZANU–PF kuanza kampeni ya kumtaka aongezewe muda ili amalize mipango yake ya maendeleo.
Mwaka uliopita, ZANU–PF ilipitisha azimio la kufanya marekebisho ya katiba ili kuongeza muda wa mihula ya urais. Pendekezo hilo baadaye lilipewa baraka na Baraza la Mawaziri mwezi Februari.
Hatua hiyo imezua mjadala mkubwa ndani na nje ya Zimbabwe, huku baadhi ya wakosoaji wakidai kuwa mabadiliko hayo yanaweza kudhoofisha misingi ya demokrasia na mfumo wa uchaguzi wa nchi hiyo.