
Msanii maarufu kutoka Colombia, Shakira, amesema onyesho la kwanza kabisa la ‘halftime show’ katika fainali ya Kombe la Dunia la FIFA litakuwa tukio la kihistoria litakalowaunganisha baadhi ya mastaa wakubwa zaidi wa muziki duniani.
Shakira atapanda jukwaani Julai 19 katika Uwanja wa MetLife, New Jersey, pamoja na BTS, Coldplay, Justin Bieber na Madonna, kwenye onyesho maalum la dakika 11 litakalofanyika wakati wa mapumziko ya mchezo wa fainali ya Kombe la Dunia 2026.
Akizungumza katika kipindi cha The Capital Evening Show with Jimmy Hill, Shakira alisema anafurahia kuwa sehemu ya historia hiyo baada ya pia kutumbuiza kwenye sherehe za ufunguzi wa mashindano hayo.
“Nilitumbuiza kwenye ufunguzi, na sasa natumbuiza kwenye fainali. Lazima nifikirie namna ya kufanya onyesho hili liwe tofauti na nililofanya wakati wa ufunguzi,” alisema Shakira.

Msanii huyo wa kibao cha Hips Don’t Lie alisema onyesho hilo litakuwa la kipekee kwa kuwa ni mara ya kwanza katika historia ya Kombe la Dunia kufanyika halftime show ya aina hiyo, akiahidi mashabiki burudani isiyokuwa ya kawaida.
“Itakuwa halftime show ya pamoja. Itakuwa ya kihistoria sana, wasanii watano wa ajabu… vizuri, wasanii wanne wa ajabu pamoja nami,” alisema kwa utani.
Shakira pia alieleza matumaini yake kwamba kiongozi wa bendi ya Coldplay, Chris Martin, ambaye ndiye msimamizi wa ubunifu wa onyesho hilo, ataungana nao jukwaani badala ya kubaki nyuma ya pazia.
“Natumaini Chris Martin ataimba pia,” alisema.
Alipoulizwa mashabiki wanapaswa kutarajia nini, Shakira alisema maandalizi bado yanaendelea na kwamba hata yeye mwenyewe ana hamu ya kuona jinsi onyesho hilo litakavyokuwa.
“Tutakutana wote na kupanga kila kitu. Kwa sasa, nina hamu ya kujua kitakavyotokea kama ilivyo kwa mashabiki,” alisema.
Kombe la Dunia limekuwa na nafasi ya kipekee katika maisha ya Shakira tangu alipotoa wimbo maarufu wa Waka Waka (This Time for Africa) mwaka 2010. Mwaka huu pia amepata mafanikio kupitia wimbo Dai Dai, aliouimba kwa kushirikiana na Burna Boy, ambao ni wimbo rasmi wa Kombe la Dunia 2026.
Wimbo huo umeendelea kufanya vizuri kwenye chati za muziki duniani na kuwa wimbo rasmi wa kwanza wa Kombe la Dunia kufikia nafasi ya kwanza kwenye Billboard Global Exclusive U.S. Chart.
Onyesho hilo la kihistoria litafanyika Julai 19 wakati wa mapumziko ya fainali ya Kombe la Dunia 2026, likiwa la kwanza kabisa kufanyika kwa mtindo unaofanana na halftime show ya Super Bowl.