×

Trump Aamuru Mashambulizi Mengine Iran, Mlango wa Hormuz Wazua Hofu Duniani

Marekani imefanya mashambulizi mapya dhidi ya Iran baada ya meli ya mizigo kushambuliwa katika Mlango wa Hormuz na kushika moto, tukio lililosababisha mfanyakazi mmoja kutoweka na kuongeza mvutano katika eneo hilo muhimu kwa biashara ya kimataifa.

Jeshi la Marekani kupitia Kamandi Kuu ya Marekani (CENTCOM) lilisema mashambulizi hayo yalifanyika kwa maelekezo ya Rais Donald Trump kwa lengo la kuifanya Iran iwajibike kwa mashambulizi dhidi ya meli za kibiashara zinazopita katika Mlango wa Hormuz.

Kwa mujibu wa CENTCOM, mashambulizi hayo yalilenga maeneo mbalimbali ya kijeshi ikiwemo mifumo ya makombora, mifumo ya ulinzi wa anga, maghala ya silaha, vituo vya mawasiliano na boti zinazotumiwa na Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Iran (IRGC).

Iran imekosoa vikali hatua hiyo, ikisema imeharibu juhudi za miezi kadhaa za kidiplomasia zilizokuwa zikilenga kumaliza mzozo huo.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ilidai pia kuwa Marekani imeongeza hali ya kutokuwa salama katika Mlango wa Hormuz kwa kuingilia mipango ya Iran ya kusimamia njia hiyo ya kimkakati.

Licha ya mapigano hayo, meli za kibiashara zimeendelea kutumia Mlango wa Hormuz. Maafisa wa Marekani walisema takribani meli 20 zilipita katika kipindi cha saa 24 zilizopita zikisaidiwa na ulinzi wa jeshi la Marekani, huku nyingine zikivuka bila ulinzi.

Baada ya mashambulizi ya Marekani, Iran ilijibu kwa kushambulia maeneo katika Bahrain, Kuwait, Qatar, Jordan na Oman, nchi ambazo zinahifadhi vituo vya kijeshi vya Marekani au zina uhusiano wa karibu wa kiusalama na Washington.

Vyombo vya habari vya serikali ya Iran viliripoti milipuko katika maeneo kadhaa, ikiwemo Kisiwa cha Qeshm, Bandar Abbas na Hajjiabad, huku vikikiri kuwa mashambulizi hayo yalitokea lakini vikidai hayakusababisha vifo katika baadhi ya maeneo yaliyolengwa.

Afisa mmoja wa Marekani alisema mashambulizi hayo yalilenga kupunguza uwezo wa Iran wa kushambulia meli zinazopita katika njia hiyo muhimu, ambayo hupitisha takribani asilimia 20 ya mafuta na gesi asilia inayouzwa duniani.

Wakati huo huo, mazungumzo kati ya Tehran na Washington kuhusu makubaliano ya muda ya siku 60 yanayolenga kumaliza vita yako hatarini kuvunjika kutokana na kuongezeka kwa mashambulizi kati ya pande hizo mbili.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, ameonya kuwa kurejea kwa vita kamili kutakuwa na athari kubwa kwa usalama wa eneo la Mashariki ya Kati na uchumi wa dunia.

Ingawa Iran imetangaza kuwa Mlango wa Hormuz umefungwa hadi hali itakapotulia, Marekani imepinga madai hayo na kusisitiza kuwa njia hiyo bado ipo wazi kwa usafiri wa kimataifa, japokuwa idadi ya meli zinazopita imepungua kutokana na hatari za kiusalama.

Leave a Comment