
Klabu ya Simba SC imetangaza kwa masikitiko kifo cha Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano, Iddi Kajuna, kilichotokea usiku wa kuamkia leo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Kupitia taarifa rasmi, Simba SC imesema Kajuna amefariki dunia akiwa bado analitekeleza jukumu lake ndani ya klabu, ambapo alikuwa akihudumu kama Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano hadi mauti yalipomkuta.
Miongoni mwa majukumu yake ya mwisho ni kushiriki katika maandalizi ya fainali ya Kombe la CRDB iliyofanyika visiwani Pemba Julai 4 mwaka huu.
Marehemu Kajuna alikuwa mmoja wa viongozi waliotoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Simba SC. Aliwahi kuwa Mjumbe wa Baraza la Ushauri la klabu chini ya aliyekuwa Rais wa Simba, Mohammed Dewji, pamoja na kushika nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa klabu mwaka 2017.
Aidha, aliwahi kuwa Mjumbe wa Kamati ya Utendaji kuanzia mwaka 2014 hadi 2018 na baadaye kuwa Mjumbe wa Bodi ya Mpito ya Wakurugenzi mwaka 2018 wakati wa maboresho ya mfumo wa uongozi wa Simba SC.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mwili wa marehemu utaswaliwa katika Msikiti wa Maamur, Upanga, na baadaye kuzikwa katika Makaburi ya Kisutu jijini Dar es Salaam leo saa 10:00 alasiri.
Simba SC imetoa salamu za pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa, marafiki na wanachama wote wa klabu, huku ikimuombea Mwenyezi Mungu amsamehe dhambi zake na ailaze roho yake mahali pema peponi.
