
Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, amewasili Ikulu ya White House mjini Washington kwa mazungumzo ya ana kwa ana na Rais wa Marekani, Donald Trump, huku vita na mvutano unaohusisha Iran vikitarajiwa kuwa ajenda kuu ya kikao hicho.
Huu ni mkutano wa nane kati ya viongozi hao tangu Trump arejee madarakani mwanzoni mwa mwaka 2025. Mazungumzo hayo yanafanyika wakati Marekani ikisema inataka kutoa nafasi kwa mazungumzo ya kidiplomasia baada ya mapigano yaliyohusisha mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran kusitishwa kwa muda.
Kabla ya kuondoka Israel kuelekea Marekani, Netanyahu alisema lengo kuu la ziara hiyo ni kujadili masuala muhimu ya usalama, hususan Iran, pamoja na kupanua ushirikiano wa amani katika eneo la Mashariki ya Kati.
“Tutajadili masuala yote yaliyo kwenye ajenda, kwanza kabisa Iran. Lengo letu ni kulinda usalama wetu na pia kupanua wigo wa amani katika eneo letu,” alisema Netanyahu.
Mbali na suala la Iran, viongozi hao wanatarajiwa kujadili utekelezaji wa makubaliano yaliyodhaminiwa na Marekani kati ya Israel na Lebanon, ambayo yalisainiwa mwezi uliopita lakini yamekuwa yakikabiliwa na changamoto katika utekelezaji wake.
Mazungumzo hayo pia yanatarajiwa kugusia hali ya Ukanda wa Gaza, ambako juhudi za kidiplomasia za kuanzisha upya ujenzi wa eneo hilo bado hazijapata mafanikio, huku hali ya kibinadamu ikiendelea kuwa ngumu.
Ziara ya Netanyahu pia imekuja wakati yeye na Trump wakijiandaa na mitihani muhimu ya kisiasa baadaye mwaka huu, ambapo Israel inatarajia kufanya uchaguzi mkuu, huku Marekani ikielekea kwenye uchaguzi wa katikati ya muhula (midterm elections).
Aidha, baada ya kuwasili Washington, Netanyahu alihudhuria chakula cha kumbukumbu kwa heshima ya marehemu Seneta Lindsey Graham na anatarajiwa kushiriki ibada ya kumbukumbu yake baadaye.