×

Iran Yazionya Nchi za Ghuba Kuhusu Mashambulizi ya Marekani

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araqchi.

Iran imezitahadharisha nchi za Ghuba kuwa shambulio lolote jipya la Marekani dhidi ya ardhi yake litajibiwa kwa mashambulizi yatakayolenga miundombinu muhimu ya nishati katika eneo hilo, hatua inayoongeza hofu ya kuongezeka kwa mvutano katika Mashariki ya Kati.

Kwa mujibu wa vyanzo kadhaa vinavyofahamu mazungumzo hayo, ujumbe huo ulitolewa kupitia mawasiliano ya ngazi za juu ya kidiplomasia baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kutishia mwishoni mwa Julai kushambulia sekta ya nishati na miundombinu ya Iran.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araqchi, anaripotiwa kufanya mazungumzo na mawaziri wenzake wa Saudi Arabia, Qatar na Uturuki, pamoja na Mkuu wa Jeshi la Pakistan, akiwataka washirika wa Marekani katika eneo la Ghuba kutumia ushawishi wao kumshawishi Trump kuachana na mpango wa kufanya mashambulizi mapya dhidi ya Iran.

Kwa mujibu wa mwanadiplomasia mmoja wa ngazi ya juu katika eneo hilo, Araqchi alisisitiza kuwa Iran iko tayari kujibu mashambulizi yoyote, lakini bado inaamini kuwa suluhisho la kidiplomasia ndilo njia bora ya kuzuia vita vikubwa zaidi.

“Tuko tayari kujibu, lakini suluhisho la kidiplomasia ndilo njia bora ya kuzuia kuongezeka kwa mapigano na uharibifu katika eneo hili,” chanzo hicho kilinukuliwa kikisema.

Chanzo kingine kutoka nchi za Ghuba kilisema Iran iliweka wazi kwamba iwapo Marekani itashambulia miundombinu yake, italenga vituo vya nishati, visafishaji vya mafuta, gridi za umeme, miundombinu ya maji, mitandao ya usafiri na maeneo ya uzalishaji wa mafuta katika nchi za Ghuba.

Hatua hiyo inaonekana kuwa sehemu ya mkakati wa Tehran wa kuongeza gharama za kisiasa na kiuchumi kwa Marekani na washirika wake wa eneo hilo endapo kutazuka mashambulizi mapya.

Baada ya ujumbe huo, Mwanamfalme wa Saudi Arabia, Mohammed bin Salman, anaripotiwa kuzungumza na Rais Trump na kumhimiza kuahirisha hatua yoyote ya kijeshi, kurejea kwenye mazungumzo na kutafuta suluhisho la kidiplomasia badala ya kuongeza mvutano.

Aidha, Qatar, Oman na Saudi Arabia zimeendelea kuhimiza Marekani kuanzisha tena mazungumzo na Iran ili kuepusha mzozo mpya ambao unaweza kuhatarisha usalama wa eneo la Ghuba na kuathiri usambazaji wa nishati duniani.

Kwa mujibu wa mmoja wa maofisa wa Iran, Tehran inaamini kuwa shambulio lolote jipya dhidi yake litazua athari kubwa kwa uchumi wa mataifa ya Ghuba na usambazaji wa mafuta duniani, jambo ambalo linaweza kulazimisha pande husika kurejea mezani kwa mazungumzo.

Hata hivyo, mwanadiplomasia mmoja wa eneo hilo alisema changamoto kubwa inayobaki ni kwamba Marekani inataka makubaliano ambayo inaweza kuyaonyesha kama ushindi wake, huku Iran nayo ikitaka kulinda hadhi yake na maslahi yake ya kimkakati.

Leave a Comment