
Rais wa Marekani, Donald Trump, ametia saini amri mbili mpya zinazolenga kubadili utekelezaji wa haki ya uraia wa kuzaliwa nchini humo, hatua inayolenga kuzuia baadhi ya watoto wanaozaliwa Marekani kupata uraia wa moja kwa moja.
Amri ya kwanza inalenga kupunguza idadi ya watoto wa raia wa kigeni wanaopata uraia wa Marekani kwa kuzaliwa, huku amri ya pili ikilenga kile kinachojulikana kama “utalii wa kujifungua” — hali ambapo wanawake wajawazito husafiri kwenda Marekani kwa lengo la kujifungua ili watoto wao wapate uraia wa Marekani.
Akizungumza katika Ofisi ya Oval, Trump alisema hatua hiyo ilipaswa kuchukuliwa muda mrefu uliopita na kwamba utawala wake unalenga kushughulikia suala hilo.
“Hatua hii ilipaswa kuchukuliwa miaka mingi iliyopita, lakini sasa tunatatua tatizo hili,” amesema Trump.
Rais huyo pia ameikosoa Mahakama Kuu ya Marekani kwa kukataa jaribio lake la awali la kubadili mfumo wa uraia wa kuzaliwa, ambao umekuwepo kwa takribani miaka 150.
Kwa mujibu wa amri hizo mpya, baadhi ya watoto wanaozaliwa Marekani hawatapata uraia wa moja kwa moja endapo wazazi wao wote wawili si raia wa Marekani na mmoja wao atakuwa:
- Mwanachama wa kundi la kigaidi la kigeni;
- Mfanyakazi wa serikali ya kigeni;
- Amepata au kujaribu kupata uraia wa Marekani kwa njia ya udanganyifu;
- Anaishi katika maeneo ambayo hayatoi uraia wa kuzaliwa chini ya sheria za shirikisho.
Hata hivyo, uraia wa watu wanaozaliwa katika maeneo ya Marekani kama Puerto Rico utaendelea kutambuliwa chini ya sheria za shirikisho.
Trump na maafisa wa utawala wake wamekuwa wakikosoa mara kwa mara utalii wa kujifungua, wakidai kuwa baadhi ya nchi hutumia mfumo huo kupata manufaa ya uraia wa Marekani.
Hata hivyo, utafiti wa taasisi huru ya Migration Policy Institute unaonyesha kuwa idadi ya watoto wanaozaliwa Marekani kupitia utalii wa kujifungua inakadiriwa kuwa kati ya 22,000 na 26,000 kwa mwaka.