
DUBAI: Nyota wa Al-Nassr, Cristiano Ronaldo, na mpenzi wake wa muda mrefu, Georgina Rodriguez, wamefunga ndoa baada ya kuwa kwenye uhusiano kwa takribani muongo mmoja.
Ronaldo mwenye umri wa miaka 41, alithibitisha taarifa hizo kupitia ukurasa wake wa Instagram kwa kushiriki picha ya pete za ndoa za wawili hao na kuambatanisha ujumbe mfupi, “C❤️G.”
Kwa mujibu wa taarifa zilizochapishwa na Daily Mail, wawili hao walifunga ndoa katika hafla ya faragha iliyofanyika Cascais, nchini Ureno, na kuhudhuriwa na watoto wao watano.

Mwakilishi wa Ronaldo pia alithibitisha ndoa hiyo, akisema wawili hao sasa ni “mume na mke rasmi.”
Ndoa hiyo imekuja mwaka mmoja baada ya Georgina kutangaza uchumba wao kwa kuonyesha pete kubwa ya almasi yenye umbo la mviringo kwenye Instagram.
“Yes I do. In this and in all my lives,” aliandika Georgina wakati huo.
Ronaldo na Georgina walikutana mwaka 2016 mjini Madrid, Hispania, wakati Georgina alipokuwa akifanya kazi katika duka la Gucci. Uhusiano wao uliwekwa wazi kwa umma mwaka mmoja baadaye.
Wawili hao wana watoto wawili pamoja, Alana Martina na Bella Esmeralda. Georgina pia amekuwa akimlea Cristiano Jr. pamoja na mapacha Eva na Mateo, ambao Ronaldo aliwapata kabla ya uhusiano wao.

Mwaka 2022, Ronaldo na Georgina walitangaza kwa masikitiko kifo cha mtoto wao wa kiume, Angel, aliyefariki wakati wa kujifungua, huku pacha wake Bella Esmeralda akinusurika.
Uhusiano wa Ronaldo na Georgina umekuwa ukifuatiliwa kwa karibu na mashabiki duniani, hasa baada ya Ronaldo kuhamia Saudi Arabia mwaka 2023 kujiunga na Al-Nassr.
Georgina amekuwa akishirikisha maisha yao ya kifamilia kupitia mitandao ya kijamii na pia katika kipindi chake cha Netflix, “I Am Georgina.”
Kabla hata ya uchumba wao kutangazwa rasmi, kulikuwa na uvumi wa ndoa. Mwaka 2024, Ronaldo aliwahi kumtaja Georgina kama “mke wangu” alipokuwa akizungumzia mazoezi yao ya nyumbani, lakini wakati huo mwakilishi wake hakuthibitisha kama walikuwa wamefunga ndoa.