
Baada ya Jopo la Majaji watatu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dar es Salaam, kumkuta Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Tundu Antiphas Lissu, ana kesi ya kujibu katika shauri la uhaini namba 19605/2025, utetezi wake umeanza rasmi leo, Agosti 21, 2026.
Kesi hiyo iliendelea saa 9:48 Alasiri baada ya mahakama kutoa mapumziko mafupi. Jopo la majaji lilipoingia ukumbini, upande wa mashtaka ulieleza kuwa uko tayari kusikiliza utetezi wa Lissu, huku yeye pia akithibitisha kuwa yuko tayari kuanza kutoa ushahidi.
Kabla ya kuanza utetezi, Lissu aliomba maelekezo kuhusu utaratibu wa mashahidi wake ambao wamepangwa kutoa ushahidi, akitaka kujua kama wanapaswa kubaki ndani ya ukumbi au kutoka nje.
Majaji walielekeza kuwa mashahidi wengine hawapaswi kuwepo ndani ya ukumbi wakati shahidi mwingine akitoa ushahidi.
Kutokana na maelekezo hayo, viongozi waandamizi wa CHADEMA waliopangwa kuwa mashahidi, akiwemo John Mnyika, Amani Golugwa na John Heche, waliondoka ukumbini kusubiri kuitwa kutoa ushahidi wao.

Baada ya hapo, Lissu alisimama kizimbani na kula kiapo kama shahidi wa kwanza wa utetezi.
Akianza ushahidi wake, Lissu alisema sehemu ya kwanza ya utetezi wake inahusu maisha yake binafsi, akieleza kuwa maelezo hayo yatasaidia mahakama kumuelewa yeye ni mtu wa aina gani.
Lissu alijitambulisha kama kiongozi wa chama cha siasa kilichosajiliwa kisheria na kueleza kuwa amekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa tangu Januari 22, 2025.
Alisema alidumu katika nafasi hiyo kwa takribani wiki tano au sita kabla ya kukamatwa na kufunguliwa mashtaka ya uhaini.
Katika ushahidi wake, Lissu pia alieleza historia ya uongozi wake ndani ya CHADEMA, akibainisha kuwa aliwahi kuwa Naibu Mwenyekiti wa CHADEMA Bara kwa kipindi cha miaka mitano, kuanzia Desemba 2019 hadi Januari 22, 2025.
Aidha, alieleza kuwa aliwahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA na Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama kuanzia mwaka 2010 hadi Septemba 7, 2017.
Utetezi wa Lissu sasa unaendelea mbele ya jopo hilo la majaji, huku akianza kueleza historia yake binafsi na kisiasa kama sehemu ya ushahidi wake katika kujibu mashtaka yanayomkabili.
Baada ya kuanza kutoa ushahidi wake leo, shauri hilo limeahirishwa hadi Jumatatu, Agosti 24, 2026 kwa ajili ya kuendelea na ushahidi wa utetezi.