×

Dkt. Gwajima Aingilia Kati Sakata la Mobetto, Aonya Ukatili Mtandaoni

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima, ametoa ujumbe wa kuunga mkono mapambano dhidi ya ukatili mtandaoni, huku akimpongeza msanii na mrembo Hamisa Mobetto kwa kuzungumzia changamoto hiyo hadharani.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Dkt. Gwajima amesema anatoa pole kwa watu wote waliofanyiwa au wanaoendelea kufanyiwa ukatili mtandaoni, akisisitiza umuhimu wa waathirika kutafuta msaada na kuchukua hatua stahiki.

Dkt. Gwajima pia amempongeza Hamisa Mobetto kwa kupaza sauti kuhusu suala hilo na kueleza kuwa yuko tayari kumsaidia kupata wataalamu watakaoweza kumsikiliza na kumpa ushauri.

Aidha, Waziri huyo ametoa onyo kwa watu wanaodaiwa kuhusika na vitendo vya kumkatili Hamisa, akiwataka kutambua kuwa umaarufu na nafasi walizonazo havipaswi kutumiwa kuvuruga amani na ustawi wa wengine.

“Hivi mnaona raha sana kutumia fursa mlizonazo kuvunja amani za wengine? Hivi umaarufu wenu unafanyika kioo cha jamii au giza la jamii?” amehoji Dkt. Gwajima.

Amesema tabia za aina hiyo zinaweza pia kuibua masuala ya kisheria, akiwataka wanaokumbana na ukatili mtandaoni kutumia njia zinazotambulika kisheria, ikiwemo kutoa taarifa kwa vyombo husika na kupata msaada wa mawakili.

Dkt. Gwajima ameendelea kusisitiza umuhimu wa maadili katika matumizi ya mitandao ya kijamii, akisema maadili mabaya yanaweza kuwa na madhara makubwa kwa mtu binafsi na jamii kwa ujumla.

Amehoji pia namna ambavyo baadhi ya wanajamii hushiriki au kushabikia maudhui yanayowajadili na kuwashambulia watu wengine, lakini wanapokumbwa na hali kama hiyo wao wenyewe hukimbilia kuomba msaada.

“Jamii bila maadili ni majanga na misiba. Tushirikiane kujenga maadili mema,” amesema.

Katika ujumbe wake, Dkt. Gwajima amesisitiza kuwa waathirika wa ukatili mtandaoni hawapaswi kukaa kimya, bali wanapaswa kutumia fursa zilizopo za kisheria na kupata msaada wa kitaalamu ili hatua zichukuliwe dhidi ya wanaokiuka sheria.

Akiuhitimisha ujumbe wake kwa msisitizo, Waziri huyo ameuliza: “Niongeze sauti au imetosha?” huku akiahidi kuendelea kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa maadili na matumizi salama ya mitandao ya kijamii.

Leave a Comment