×

Rais Samia Aondoka Nchini Kwenda Zambia Kwa Uapisho Wa Hichilema

Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiagana na Viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume Zanzibar kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Luzaka Zambia kuhudhuria Sherehe za Uapisho wa Rais Mteule wa Jamhuri ya Zambia Mheshimiwa Hakainde Hichilema kufuatia ushindi alioupata katika Uchaguzi Mkuu wa Zambia Uliofanyika tarehe 13 Agosti, 2026 ambapo Rais Hichilema alichaguliwa kwa Muhula mwengine wa Miaka mitano. Tarehe 01 Sept, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Septemba 1, 2026, ameondoka nchini kuelekea Lusaka, Zambia, kushuhudia sherehe za uapisho wa Rais wa Zambia, Hakainde Hichilema.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Rais Hichilema alichaguliwa tena katika Uchaguzi Mkuu wa Zambia uliofanyika Agosti 13, 2026, na amechaguliwa kuongoza nchi hiyo kwa muhula mwingine wa miaka mitano. Taarifa nyingine pia zimethibitisha kuwa uapisho huo umepangwa kufanyika Septemba 1, 2026.

Ziara ya Rais Samia nchini Zambia inaelezwa kuwa sehemu ya kuendeleza uhusiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Zambia, unaojengwa katika misingi ya umoja, mshikamano, ujirani mwema na ushirikiano wa kikanda.

Uhusiano kati ya Tanzania na Zambia umeendelea kuwa muhimu katika maeneo mbalimbali, ikiwemo biashara, usafirishaji na miundombinu, huku mataifa hayo yakishirikiana pia katika masuala ya maendeleo ya kikanda.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari S. Machumu.

Leave a Comment