




MKUU wa Wilaya ya Kinondoni, Ali Hapi leo katika ziara yake ya kutembelea wananchi wa wilaya yake ametoa mwezi mmoja kwa mwekezaji wa soko la Makumbusho kuhakikisha analipa deni lote analodaiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni zaidi ya milioni 80.
Akizungumza na wakazi wa Makumbusho wakiwemo wafanyabiashara ndogondogo wa kituo cha daladala, mbali na kutoa muda huo, pia alisikiliza tuhuma mbalimbali zilizotolewa na wafanyabiashara ndogondogo zikilenga uongozi wa soko kuwanyanyasa wafanyabiashara wa maeneo hayo . Hapi amesema lazima asikilize kero za wananchi wa wilaya yake kwani cheo alichonacho ni kwa ajili ya kusikiliza shida zao.
Amesema hawezi kukubaliana mwekezaji asiyelipa kodi kama mikataba inavyosema hivyo atalazimika kuivunja ili kutafuta mwekezaji mwingine ambaye atakuwa akitekeleza mikataba watakayokubaliana.
Mmoja wa wafanyabiashara ndogondogo katika soko la Makumbusho alielezea namna ambavyo wanafanya biashara zao kwa manyanyaso makubwa na kunyang’anywa biashara zao ambazo hupelekwa ofisi ya Mwekezaji, vitendo vinavyofanywa na mabaunsa waliopo sokoni hapo, ambapo akijibu malalamiko ya vijana wanaonyanyaswa ameagiza uongozi wa soko hilo kuhakikisha wale wote waliotuhumiwa kwa kuwanyanyasa wafanyabiashara wa eneo hilo watafutwe mara moja ili waweze kujibu tuhuma zinazowakabili.
HABARI: DENIS MTIMA/GPL