
BENCHI la ufundi la timu ya Singida United ya Singida chini ya kocha wake mkuu, Hans van Der Pluijm, raia wa Uholanzi, limejinasibu kuivunja rekodi ya Mtibwa Sugar ya kutofungwa kwenye michezo yao saba ya Ligi Kuu Bara hadi sasa kwa kuwafunga kwenye mechi itakayopigwa wikiendi hii mkoani Morogoro.
Singida United wenye pointi 12 kwenye msimamo wa ligi watakuwa wageni wa Mtibwa Sugar wenye pointi 15 ambao hawajapoteza mchezo wowote kwenye ligi, kwenye mechi itakayopigwa Jumamosi hii katika Uwanja wa Manungu mkoani Morogoro.

Akizungumza na Championi Jumatano, Mholanzi huyo amesema kuwa wapo tayari kwa ajili ya kuvaana na wapinzani wao huku wakiwa na shauku kubwa ya kupata pointi tatu baada ya kushindwa kufanya hivyo kwenye mechi iliyopita waliyokuwa ugenini dhidi ya Ndanda FC ya Mtwara.
“Tunataka kushinda mechi hii na Mtibwa Sugar kwa sababu mechi iliyopita hatukufanya vizuri na tukaambulia pointi moja pekee tukiwa kule Mtwara, safari hii tunataka tupate pointi zote tatu na wachezaji wako tayari kwa ajili ya hilo.
“Tunatambua kwamba wapinzani wetu wako vizuri kwa sababu hawajapoteza kwenye mechi zao hadi sasa, lakini hilo haliwezi kuwa sababu ya sisi eti tukashindwa kupata pointi kwani tunaingia uwanjani tukiwa na lengo moja pekee la kushinda na siyo jambo lingine,” alisema kocha huyo.