×

Kombinesheni Ya Ajibu, Chirwa Moto Chini

Ibrahim Ajibu (katikati) akifanya yake.

KATIKA kuhakikisha anapunguza tofauti ya idadi ya mabao waliyonayo dhidi ya wapinzani wao wa jadi, Simba, Kocha Mkuu wa Yanga, George Lwandamina amewapa mbinu mbadala washambuliaji wake tegemeo Ibrahim Ajibu na Obrey Chirwa.

 

Hatua hiyo imekuja ikiwa ni saa chache kab­la ya mchezo wao wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Singida United utakaopigwa kesho Jumamosi kwenye Uwanja wa Namfua mkoani Singida.

 

Simba hadi hivi sasa tayari imefanikiwa kufun­ga mabao 20 huku ikiruhusu mabao matano na Yanga ikifunga mabao 11 na kufungwa manne katika mechi nane walizocheza za ligi hiyo kwa msimu huu.

Wachezaji wa Yanga wakipongezana.

Kocha huyo alionekana akiwapa mbinu hizo kwenye mazoezi ya mwisho yaliyofanyika juzi Jumatano asubuhi kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar kabla ya kuelekea Singida kuvaana na wap­inzani wao hao.

 

Katika mazoezi hayo, Lwandamina alionekana akiwapa mbinu za kufunga washambuliaji wake hao kwa kufunga mipira ya krosi kwa njia ya kichwa na miguu kumchambua kipa.

 

Lwandamina aliwataka Ajibu na Chirwa ku­funga mabao ya umbali tofauti ya mita 20 na 18 kwa kupiga mashuti na kumchambua kipa aliyekuwepo golini ambaye ni Beno Kakolanya.

 

Mzambia huyo aliwatumia mabeki wa pembe­ni Hassan Kessy, Gadiel Michael na viungo wa pembeni, Pius Busitwa na Geofrey Mwashiuya kwa ajili ya kupiga mipira ya krosi kwa washam­buliaji hao.

 

Wakati mwingine kocha huyo, alionekana ku­tumia mbinu za kufunga wakitumia njia ya ka­tikati kupenya safu ya ulinzi ya kati akimtumia Raphael Daudi, Kabamba Tshishimbi na Ajibu kumtengenezea pasi za mabao Chirwa.

 

Kocha huyo, alitumia programu hiyo ya maz­oezi kwa saa mbili, yalianza saa 3:00 na kumal­izika saa 5:00 asubuhi.

Akizungumzia mchezo dhidi ya Singida, Lwan­damina alisema: “Kikubwa tumejipanga vema kuhakikisha tunashinda mechi na Singida ili tu­jiweke katika nafasi nzuri kwenye msimamo wa ligi kuu.

 

“Kitu kikubwa tunachotakiwa kukifanya ni ku­tumia vema kila nafasi tutakayoipata ya kufun­ga mabao ili tupate ushindi, kwani mechi iliyo­pita na Simba tulipoteza nafasi nyingi.”

Stori: Wilbert Molandi na Musa Mateja

Huyu Hapa Uwoya Akikanusha Kuolewa na Dogo Janja!!

Leave a Comment